Na Winfrida Mtoi
KIKOSI cha Simba kimekamilisha maandalizi ya mchezo wake wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Ruvu Shooting utakaopigwa Ijumaa Novemba 19,2021 kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, jijini Mwanza.
Mchezo huo utakuwa wa kwanza kwa kocha mkuu wa kikosi hicho, Pablo Franco aliyejiunga na timu hiyo hivi karibuni akichukua nafasi ya Didier Gomes.
Pia kocha mpya wa viungo Mhispania, Don Daniel De Castro ameungana na kikosi hicho baada ya kuanza mazoezi jana jioni.
Katika msimamo wa ligi hiyo, Simba inashika nafasi ya pili na pointi 11, nyuma ya watani wao Yanga wenye alama 15.
Ruvu Shooting wanayokutana nayo, ipo nafasi ya 10 na pointi sita, ikicheza mechi tano.