MAKAMU wa Rais, Samia Suluhu Hassan amesema vijana wakiamua kuchapa kazi, Tanzania haiwezi kuwa tegemezi.
Samia ameyasema hayo jana,baada ya kukagua kikundi cha vijana cha Umoja wa Mafundi Seremala kilichoko Kata ya Sabasaba mkoani Morogoro.
Alisema Serikali inapata mapato kutoka kwa wananchi na kwamba vijana wanapaswa kutumia muda mwingi kufanya shughuli zinazoleta tija ili kupunguza utegemezi wa ufadhili wenye masharti na manyanyaso mengi.
“Nawaomba vijana wa Morogoro, pool zichezwe kuanzia saa 11 jioni mpaka hata saa 6 usiku, tumeidumaza nchi yetu, halafu lawama zinakwenda kwa Serikali, inapata mapato kutoka kwa wananchi.
“Tunapunguza ufadhili, una manyanyaso mengi, usipofuata masharti yao wanakata msaada…vijana tufanye kazi tuepukane na masharti na manyanyaso, tukijitegemea tutapata heshima,”alisema.
Alikipongeza kikundi hicho cha vijana chenye wanachama 182 na kuiomba Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro kukipatia eneo ili waweze kutangaza bidhaa zao.
Kwa upande wake,Waziri wa Nchi,Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Maendeleo ya Vijana na Walemavu, Jenister Mhagama aliahidi kuwapatia mafunzo vijana hao waweze kutengeneza samani za kuuza ndani na nje ya nchi.
Samia alitoa Sh milioni 10 kwa ajili ya kusaidia vijana hao kununua vitendea kazi,huku Mbunge wa Morogoro Mjini, Aziz Abood (CCM), alichangia milioni moja ili waongezee mtaji.
Katika hatua nyingine, Samia alitembelea Hospitali ya Mkoa wa Morogoro ambapo aliwapongeza watendaji wa hospitali kwa kazi kubwa ya kuhudumia wagonjwa wapatao 500 hadi 600 kwa siku.
Akizungumza na wafanyakazi wa hospitali, aliahidi kuipatia hospitali hiyo mashine ya MRI na CT-scan na kuwaagiza watumie mfumo wa kisasa wa kielectronic ili waweze kukusanya mapato mengi na hivyo kusaidia kutatua changamoto za fedha.