30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

RUVU SHOOTING YAINYUKA YANGA

Na THERESIA GASPER-DAR ES SALAAM

TIMU ya Ruvu Shooting imeifunga Yanga bao 1-0, katika mchezo wa kirafiki uliochezwa katika Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.

Katika mchezo huo, Ruvu Shooting walipata bao hilo katika dakika ya 22, kutokana na beki wa Yanga, Abdallah Hajji, kujifunga kwa kichwa wakati akiokoa mpira wa krosi iliyopigwa na Shalla Juma.

Licha ya bao hilo, Yanga walijitahidi kusaka bao la kusawazisha bila mafanikio na hadi dakika 45 za kipindi cha kwanza zinamalizika, Ruvu walikuwa mbele kwa bao hilo moja.

Kipindi cha pili Yanga walikuja kwa kasi ili kusawazisha bao hilo, ambapo katika dakika ya 49, Juma Abdul alikosa bao baada ya kutokea piga nikupige langoni mwa Ruvu Shooting, lakini alipiga mpira uliopaa juu ya goli.

Yanga hawakuishia hapo, walizidi kuliandama lango la Ruvu Shooting, ambapo katika dakika ya 62, Emmanuel Martin alipiga shuti kali lililopaa juu ya goli.

Ruvu Shooting walijibu mashambulizi hayo katika dakika ya 69, baada ya Shalla Juma kupiga shuti kali lililotoka nje.

Hadi mchezo huo unamalizika, Ruvu Shooting walitoka kifua mbele baada ya kuibuka na ushindi wa bao 1-0.

Baada ya mchezo huo, Yanga leo watasafiri kuelekea Unguja na usiku watacheza na timu ya Mlandege katika Uwanja wa Amaan, kisha keshokutwa wataelekea Pemba kuweka kambi kujiandaa na mchezo wa  Ngao ya Jamii dhidi ya watani wao, Simba, utakaochezwa Agosti 23, mwaka huu katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles