SHIRIKA la kukabiliana na ufisadi la kimataifa la Transparency International limetoa ripoti inayoonyesha vijana wa Afrika wenye umri wa kati ya miaka 18-34, wana uwezekano mkubwa wa kutoa rushwa kuliko watu wenye umri mkubwa wa zaidi ya miaka 55.
Katika kipimo chake cha kiwango cha ufisadi duniani cha mwaka 2019, shirika hilo limesema utafiti wake pia umebaini watu maskini zaidi wana uwezekano mara mbili zaidi wa kutoa rushwa – na wana uwezekano mkubwa pia wa kuwa waathiriwa wa rushwa inayosababishwa na tabia ya urasimu kuliko matajiri.
Utafiti huo wa kila mwaka ambao kwa mwaka huu ni wa 10, katika bara la Afrika umeitaja nchi ya Jamuhuri ya Kongo kuwa ndiyo yenye kiwango cha juu zaidi ikiwa na asilimia 75 ya wale waliotoa hongo kwa polisi.
Ripoti hiyo pia imeeleza kuwa raia wa kigeni pia huchangia kwa kiasi kikubwa katika kuchochea na kushiriki vitendo vya rushwa katika bara la Afrika.
Kwa sababu hiyo wametajwa kuhujumu maendeleo ya kudumu ya kikanda.
Transparency International linasema kuwa kampuni za kigeni hutoa hongo ili kupata mikataba kama vile ya haki ya uchimbaji wa madini, mikataba ya ujenzi wa miradi mikubwa na mikataba mingine.
Transparency International linasema pia kwamba matokeo ya utafiti wake yametokana na mahojiano ya ana kwa ana kati ya Septemba 2016 na Septemba 2018, yaliyofanyika kwa ushirikiano na taasisi ya utafiti wa kimaendeleo barani Afrika-Afrobarometer.