25.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Rais Magufuli akwepa safari ya nje

JohnPombeMagufuli*Waziri Majaliwa aenda kumwakilisha

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

RAIS Dk. John Magufuli ameendelea na uamuzi wake wa kutosafiri nje ya nchi huku akilazimika kutuma ujumbe wa kumwakilisha katika mikutano ya kimataifa.

Hatua hiyo inatokana na agizo lake alilolitoa Novemba 7, mwaka jana, ambapo alipiga marufuku safari za nje ya nchi kwa maofisa wa Serikali ila tu itakapokuwa lazima na kwa ruhusa ya Ikulu.

Kutokana na hali hiyo, safari hii amelazimika kumtuma Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ili akamwakilishe katika mkutano wa wakuu wa nchi za Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC), unaofanyika mjini Gaborone nchini Botswana.

 

MAJALIWA BOTSWANA

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa aliwasili nchini Botswana juzi na kupokewa na Waziri wa Mawasiliano na Uchukuzi wa nchi hiyo, Tshenolo Mabeo baada ya kuwasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Sir Seretse Khama uliopo Gaborone.

Pamoja na hilo, pia alikutana na Katibu Mtendaji wa SADC, Dk. Stergomena Tax na kufanya mazunguzo ya muda mfupi kabla ya kuanza kwa vikao hivyo.

Dk. Stergomena alikuwa Katibu Mkuu wa iliyokuwa Wizara ya Afrika Mashariki katika uongozi wa awamu ya nne chini ya Rais mstaafu Jakaya Kikwete.

 

MSIMAMO WA MAGUFULI

Mara baada ya kuingia madarakani, Rais Magufuli alitangaza kufuta safari holela za nje alizodai zimekuwa zikiligharimu taifa mabilioni ya fedha.

Hatua hiyo aliitolea uamuzi Novemba 6, mwaka jana kwa kuagiza safari zote muhimu ughaibuni ni lazima zipate ruhusa yake au ya Katibu Mkuu Kiongozi Ikulu, lengo ikiwa ni kuokoa fedha zinazoweza kutumiwa kwa shughuli nyingine za maendeleo kwa Taifa.

Akitolea mfano, alisema katika mwaka wa fedha wa 2013/2014 na 2014/2015, Taifa lilitumia zaidi ya Sh bilioni 356 kugharimia safari za nje; jambo ambalo alisema hayuko tayari kulishuhudia.

Hadi sasa, Dk. Magufuli ameshaonyesha mfano kwa kuamuru watu wanne tu kusafiri wakitokea ofisi ya ubalozi wa Tanzania nchini Uingereza kwenda kumwakilisha katika mkutano wa wakuu wa nchi za Jumuiya ya Madola uliofanyika visiwa vya Malta, badala ya watu zaidi ya 50 waliozoea kusafiri katika safari kama hii ya rais.

Mbali na kudhibiti safari za nje, Rais Magufuli na Serikali yake pia amedhibiti safari za ndani baada ya kuagiza kuwa vikao vyote vya kikazi baina ya viongozi wa mikoa vifanywe kupitia teknolojia ya video (video conference) na si kusafiri kutoka mkoa mmoja hadi mwingine au kukodi ukumbi wa mikutano.

Desemba 17, mwaka jana Rais Magufuli aliagiza kusimamishwa kazi mara moja kwa watumishi waandamizi wanne wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), ambao walisafiri nje ya nchi licha ya kupiga marufuku safari za nje kwa watumishi wa umma.

Watumishi hao ni Mary Mosha, Ekwabi Mujungu, Doreen Kapwani na Rukia Nikitas.

Agizo hilo la Rais Magufuli lilitolewa na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.

Kutokana na uamuzi huo, Balozi Sefue aliwataka watumishi wengine wa umma kutii agizo la Rais Magufuli na kuonya kuwa atakayekiuka atachukuliwa hatua kali.

Tangu alipoapishwa kushika madaraka ya urais, Dk. Magufuli amesafiri mara mbili, zote zikiwa ni safari za ndani ambapo ya kwanza alikwenda mkoani Dodoma kuhutubia Bunge na ya pili ni ya Januari 12, mwaka huu alipokwenda visiwani Zanzibar kwenye sherehe za miaka 52 ya Mapinduzi.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles