NA ESTHER MNYIKA, DAR ES SALAAM
WAKALA wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA), imeanzisha mpango maalumu wa kupima afya za wafanyakazi waliowahi kufanya kazi migodini.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Mtendaji Mkuu wa Osha, Dk. Akwilina Kayumba, alisema kumekuwapo na ukiukwaji wa Sheria ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi ya mwaka 2003, inayomtaka mfanyakazi kupima afya kabla na baada ya ajira ili kujua madhara aliyopata akiwa kazini.
Alisema mpango huo umeanza kutekelezwa na Mgodi wa Bulyahulu na hadi sasa wafanyakazi 315 kati ya 371 walioachishwa kazi mwaka 2007 wameshafanyiwa vipimo vya afya.
“Osha itaendesha mpango maalumu wa upimaji wa afya za waliokuwa wafanyakazi wa Bulyanhulu walioachishwa kazi na mgodi huo mnamo mwaka 2007 bila kupimwa afya zao kinyume cha sheria ya usalama na afya mahali pa kazi ya mwaka 2003.
“Katika kushughulikia tatizo hilo, vikao vya mashauri vilivyojumuisha Serikali, mwajiri wa Bulyanhulu na waathirika kupitia Chama cha Tamico, vilifanyika na utaratibu wa kushughulikia suala hilo umewekwa,” alisema Dk. Kayumba.
Alisema Tamico ilipewa jukumu la kuwatafuta waathirika wote popote walipo na kuwasilisha majina yao kwa Osha kuwa na jukumu la kuyapeleka majina hayo kwa mwajiri kwa ajili ya uhakiki na kuratibu upimaji afya wa waathirika hao.
Alisema baada ya ukiukwaji huo wa sheria kuripotiwa, hatua stahiki zilichukuliwa ikiwamo kufanya ukaguzi maalumu wa usalama na afya katika eneo la mgodi na kutoa onyo kali kwa mwajiri na kugharamia upimaji afya za waathirika wote.
Alisema maandalizi ya upimwaji huo yamekamilika na utafanyika katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) na katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando.