25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Ofisi ya Msajili wa Hazina kuendelea kusimamia taasisi na mashirika ya umma

Na Ramadhan Hassan, Dodoma

Ofisi ya Msajili wa Hazina imesema itaendelea kusimamia kwa karibu utendaji wa Taasisi na Mashirika ya Umma ili kuhakikisha kuwa Serikali inapata marejesho ya uwekezaji wake.

Hayo yameelezwa Oktoba 26, 2022 jijini Dodoma na Mkurugenzi wa Uwekezaji wa Umma kutoka Ofisi ya Msajili wa Hazina (OMH), Lightness Mauki wakati alipokuwa akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu utekelezaji wa majukumu ya ofisi hiyo katika kipindi cha Serikali ya awamu ya sita.

Mkurugenzi huyo amesema ofisi hiyo itaendelea itaendelea kusimamia kwa karibu utendaji wa Taasisi na Mashirika yaUmma ili kuhakikisha kuwa Serikali inapata marejesho ya uwekezaji wake

Sambamba na kuongezeka kwa mapato yasiyo ya kodi ili kusaidia miradi ya maendeleo kwa faida ya Taifa na wananchi wote kwa ujumla.

“Katika kuhakikisha azma hii inafikiwa, Ofisi itaendelea kutoa miongozo wezeshi itakayosaidia ubunifu na utekelezaji wa sheria bila mkwamo,” amesema Mkurugenzi huyo.

Amesema hadi kufikia Juni 30, mwaka huu, Ofisi ya Msajili wa Hazina ilikuwa inasimamia Taasisi na Mashirika ya Umma 287.

“Kati ya hizi kuna Mashirika na Taasisi 237 ambayo umiliki wake ni zaidi ya asilimia 51 kwa mujibu wa Sheria ya Mashirika ya Umma Sura 257, Taasisi 40 zinazomilikiwa na Serikali kwa hisa chache na Taasisi 10 za nje ya nchi,” amesema.

Amesema thamani ya uwekezaji wa serikali kwenye mashirika hayo ni Sh trilioni 70.

Amesema katika kutekeleza majukumu yake ya kisheria pamoja na mambo mengine Msajili wa Hazina ana jukumu la kukusanya mapato yasiyo ya kodi ambayo yanajumuisha Gawio, Michango ya 15% ya Mapato ghafi na mapato mengineyo.

“Ofisi imeendelea kutekeleza jukumu hili kwa ufanisi ambapo mapato yamekuwa yakiimarika mwaka hadi mwaka.

“Kufikia tarehe 30 Juni 2022, OMH ilikuwa imekusanya kiasi cha Sh bilioni 852.98 sawa na asilimia 109.5 ya lengo (lengo lilikuwa kukusanya Sh bilioni 779.03) na asilimia 33.5 zaidi ya kiasi kilichokusanywa 30 Juni 2021 ambacho kilikuwa ni Sh bilioni 638.87,” amesema.

Amesema serikali kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina imeendelea na juhudi za kusimamia utendaji wa Kampuni ambazo serikali ina umiliki wa hisa chache ikiwa ni pamoja na kufanya majadiliano na wabia wenza na kusimamia kwa karibu matumizi yasiyo ya lazima.

Aidha, Benki ya NMB imetoa kwa Serikali gawio la kiasi cha Sh bilioni 30.7 kutoka Sh bilioni 21.7 ya mwaka 2020/21.

Amesema Ofisi inaendelea kusimamia utendaji katika Kampuni ambazo serikali ina hisa chache ambapo, pamoja na mambo mengine, serikali imefanikiwa kufanya majadiliano na Wanahisa wenza kwa lengo la kuboresha utendaji wa Kampuni hizo ili kuhakikisha Serikali inapata gawio pamoja na kuongeza idadi za hisa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles