23.8 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Nooij atamba kuifunga Misri

NA MWALI IBRAHIM, DAR ES SALAAM
KOCHA Mkuu wa timu ya Taifa ‘Taifa Stars’, Mart Nooij, amewatoa hofu Watanzania kwa kuwahakikishia kuwa kikosi chake kitaibuka na ushindi dhidi ya timu ya Misri, katika mchezo wa kuwania kufuzu fainali za Mataifa Afrika (AFCON) mwaka 2017, mchezo utakaopigwa Juni 14, katika uwanja wa Borg El Arab, jijini Alexandria.

Jumla ya msafara wa watu 34 uliondoka jana kuelekea Addis Ababa, nchini Ethiopia, kuweka kambi ya wiki moja kujiandaa na mchezo huo, wakiwemo wachezaji 23, benchi la ufundi lenye watu saba na viongozi wanne wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).

Akizungumza Dar es Salaam jana, Nooij aliahidi mambo matatu, kuonyesha kandanda safi, ushindi, kufanya mambo tofauti na ilivyokuwa kwenye michuano iliyopita ya COSAFA, ili kuweza kurudi kamili kujiandaa na michuano ya CHAN dhidi ya Uganda, mchezo utakaochezwa Zanzibar.

“Tutaitumia vizuri kambi hiyo ya wiki moja kabla ya kucheza na Misri, nina imani tutaibuka na ushindi na Watanzania wategemee hilo na tuna uhakika huo,” alisema.

Wachezaji wanaosafiri kuelekea nchini Ethiopia ni Makipa Deogratias Munish ‘Dida’, Aishi Manula na Mwadini Ali.

Walinzi Shomari Kapombe, Oscar Joshua, Erasto Nyoni, Nadir Haroub, Aggrey Morris, Mwinyi Haji, Salum Mbonde na Juma Abdul.

Viungo Mwinyi Kazimoto, Abdi Banda, Salum Telela, Frank Domayo, Jonas Mkude, Said Ndemla.

Washambuliaji Saimon Msuva, John Bocco, Thomas Ulimwengu, Mbwana Samatta, Mrisho Ngasa na Juma Liuzio.

Wakati hao wakielekea Ethiopia, wachezaji waliobaki wanatarajia kuondoka nchini kesho, kuelekea nchini Rwanda kucheza mchezo wa kirafiki na timu ya taifa ya Rwanda katika kumbukumbu ya mauaji ya kimbari.

Wachezaji hao ni Peter Manyika, Said Mohamed, Emmanuel Semwanda, Joram Mgeveke, Hassan Isihaka, Gadiel Michael na Hassan Dilunga.

Wengine ni Rashid Mandawa, Atupele Green, Kelvin Friday, Hassan Kessy, Ibrahim Ajib, Malimi Busungu, Mudathir Yahya, Deus Kaseke, Andre Vicent, Amri Kiemba na Mohamed Hussein.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles