33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

NBS: Uchumi wa Tanzania umeimarika

Mkurugenzi wa takwimu za uchumi, Moris Oyuke
Mkurugenzi wa takwimu za uchumi, Moris Oyuke

NA NORA DAMIAN, DAR ES SALAAM

OFISI ya Taifa ya Takwimu (NBS) imesema katika robo ya kwanza ya mwaka huu inayoanzia Januari hadi Machi, uchumi umepanda  kwa asilimia 7.4 ikilinganishwa na asilimia 7.1 katika robo ya kwanza ya mwaka jana.

Kukua huko kwa uchumi kumechangiwa na sekta za umeme na maji, mawasiliano na uchukuzi na viwanda na ujenzi.

Akizungumza jana, Mkurugenzi wa takwimu za uchumi, Moris Oyuke, alisema sekta ya umeme na maji imekua kwa asilimia 12.6 ikilinganishwa na asilimia 6.2 ya mwaka jana wakati sekta ya mawasiliano na uchukuzi imekua kwa asilimia 16.5 na sekta ya viwanda na ujenzi imekua kwa asilimia 8.1.

“Taarifa zilizotumika kutayarisha takwimu hizi zimetokana na uzalishaji wa bidhaa na huduma nchini katika kipindi cha robo ya kwanza ya mwaka huu. Ukokotoaji wa takwimu hizi umezingatia matakwa ya mfumo wa Umoja wa Mataifa wa ukokotoaji takwimu za pato la taifa,” alisema Oyuke.

Alisema shughuli za kiuchumi za kilimo cha mazao zimekua kwa asilimia 1.4 ikilinganishwa na asilimia 0.6 mwaka jana wakati shughuli za uvuvi zimekua kwa asilimia 2.5 ikilinganishwa na asilimia 1.8 ya mwaka jana.

Kwa mujibu wa mkurugenzi huyo, kasi ya ukuaji huo ilitokana na kuongezeka kwa uvunaji wa samaki ili kukidhi mahitaji katika soko la ndani na soko la kimataifa.

Pia alisema ukuaji wa uchumi katika kipindi cha Januari hadi Desemba mwaka huu, unatarajiwa kufikia asilimia 7.2. Mwaka jana uchumi ulikua kwa asilimia 7.0.

Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Sera na Mipango kutoka Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika, Oswald Ruboha, alisema kukua kwa sekta ya kilimo kumechangiwa na msimu wa vuli wa mwaka jana kuliko ule wa mwaka juzi.

Mhadhiri wa Uchumi kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk. Stephen Kirama, alisema kutokana na kuwapo kwa malalamiko kwamba uchumi unakua bila kupunguza umaskini, ni vyema kwa watunga sera na wanaozisimamia kuangalia ni maboresho gani yanahitajika hasa kwa sekta zinazofanya vizuri.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles