23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

MWILI WA BALOZI MWAMBULUKUTU WAAGWA DAR

MARGRETH MWANGAMBAKU(TUDARCO) Na TUNU NASSOR

DAR ES SALAAM

WAZIRI wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya makazi, William Lukuvi amewaongoza mamia ya waombolezaji kuuaga mwili wa aliyekuwa balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini, Emmanuel Mwambulukutu.

Balozi Mwambulukutu alifariki dunia Agosti 13, mwaka huu nyumbani kwake Mikocheni jijini Dar es Salaam baada ya kusumbuliwa na ugonjwa wa kisukari kwa muda mrefu.

Viongozi wengine waliokuwa katika msiba huu ni Mbunge na Mke we Rais Mstaafu Mama Salma Kikwete , Waziri Mkuu Mstaafu Jaji Joseph Warioba,  Mbunge wa zamani wa Lupa, Njelu Kasaka,  Philip Magani pamoja na Jaji Mstaafu  Damian Lubuva.

Akizungumza wakati wa kuaga mwili huo, Waziri Lukuvi alisema marehemu Mwambulukutu atakumbukwa kwa uchapakazi wake kwani ndiye aliyeanzisha ubalozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini.

“Nilimpenda kwa kuwa alikuwa mwadilifu na jasiri na hajawahi kuwa na rekodi ya kugombana na mtu yeyote na alikuwa mwanadiplomasia kabla hata ya kuwa balozi,” alisema Lukuvi.

Akimzungumzia marehemu, mke wa Rais Mstaafu Salma Kikwete,  alisema Mwambulukutu alikuwa ni mtu mwenye imani na aliyependa familia.

“Wakati mzee (Rais Jakaya Kikwete) akiwa waziri yeye alikuwa naibu waziri hivyo tuliishi naye kama familia, nimekuja kumpa pole mke wa marehemu kama dada yangu kwa kufiwa na mumewe,” alisema Mama Salma.

Kwa upande wake Njelu Kasaka alisema Mwambulukutu alikuwa anajituma kazini na hakuwahi kuwa na mgogoro na mtu.

“Alikuwa mcheshi na mwenye kujituma na hajawahi kuingia katika mgogoro na mtu hadi umauti unamfika,”  alisema Kasaka.

Marehemu Mwambulukutu alizaliwa Novemba 22, 1944 Tukuyu Mkoani Mbeya na ameacha mjane na watoto wanne.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles