Na Kulwa Mzee, Dar es Salaam
IDARA ya Uhamiaji imesema mwanamkakati wa aliyekuwa mgombea urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Bashir Awale, amekiuka masharti ya kibali cha ukaaji alichopewa.
Kamishna wa Uhamiaji, Usimamizi na Udhibiti wa Mipaka nchini, Abdullah Abdullah alisema hayo jana alipotoa ufafanuzi kuhusu hatua ya polisi kumkamata Awale Jumatatu iliyopita.
“Hati yake ni ya ukaaji …inampa sifa ya mgeni aliyeruhusiwa kuishi nchini kwa kazi ya uwekezaji na wala siyo kujihusisha na siasa.
“Mgeni kujihusisha na masuala ya siasa ni kinyume cha katiba na sheria za nchi, Awale amekiuka masharti ya kibali cha ukaaji alichopewa na uhamiaji,”alisema.
Kibali chake cha ukaaji cha Awale kinaonyesha ni namba 008629, RPA 1004476 na kilitolewa kwa mujibu wa Sheria ya Uhamiaji ya Mwaka 1995, kifungu namba 19.
Awale ambaye ni Mkenya, kibali chake Class (Daraja) A kilitolewa kwa miaka mwili na kinaisha Desemba 12,2015. Kilikuwa ni kwa ajili ya ajira maalum katika Kampuni ya Capital Advisors Ltd.
Kibali hicho kilikuwa na masharti zaidi ya manne ikiwamo kusihi Dar es Salaam, kufanya kazi Dar es Salaam na kutoruhusiwa kujiingiza katika ajira nyingine na biashara zaidi ya nafasi yake ya ukurugenzi.
Masharti mengine ni kwamba mke na mtoto ambao hawamo katika kibali hicho hawaruhusiwi kujiingiza katika ajira yoyote.
Vilvile kibali hicho kinaonyesha Awale ana hati ya kusafiria namba C000529 iliyotolewa Kenya Julai 7,2008.
Inadaiwa Awale alikamatwa Jumatatu jioni Mikocheni Dar es Salaam baada ya kusimamamishwa na askari waliomchukua katika gari lao huku wakilitelekeza gari lake eneo hilo.