31.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Mshikemshike

magufuli* Tume ya Uchaguzi yakana tuhuma za Freeman Mbowe

* Dk. Magufuli asema CCM haiwezi kung’oka kama jino

* Lowassa aonya asema kuyakataa mabadiliko ni kujiandalia tabu

Na Waandishi Wetu

WAKATI zikiwa zimebaki siku 26 kabla ya kufanyika kwa uchaguzi mkuu, kampeni za wagombea urais zinaonekana kushika kasi katika mikoa mbalimbali nchini.

Wakati vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), vikisema mwisho wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) umewadia, mgombea wa chama hicho Dk. John Magufuli amesema CCM haiwezi kung’oka madarakani kama jino.

Naye Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe aliibua tuhuma dhidi ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), akisema kitendo cha wakurugenzi wa tume hiyo kuhamishwa ni mkakati wa kutaka kuibeba CCM.

Hata hivyo tume hiyo ya uchaguzi imekanusha madai hayo na kusema hakuna mtumishi wake aliyehamishwa kwa ajili ya kutaka kuhujumu uchaguzi wa mwaka huu.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Mwenyekiti wa NEC, Jaji Damian Luvuba alisema hadi sasa hakuna mkurugenzi yeyote aliyehamishwa tofauti na mabadiliko yaliyofanywa na Rais Jakaya Kikwete katika nafasi ya Mkurugenzi wa Uchaguzi kwa kumteua Julius Malaba kuwa jaji.

“Nakwambia ndugu yangu, Mbowe na Chadema waache kutapatapa…wanaingilia utendaji kazi wa tume na Serikali, nawaomba wasiendelee kupotosha umma.

“Hii si mara ya kwanza kuibuka na madai haya, wanazungumzia wizi wa kura kila siku, waiachie tume ifanye kazi zake, hakuna wizi wa kura wowote ule tunaongozwa na sheria za nchini,”alisema Jaji Lubuva.

“Nipo njiani natoka Arusha, nimekutana na wanasheria wa nchi jana (juzi) na pale alikuwapo kiongozi mmoja wa Chadema akawa anazungumzia malalamiko haya haya…nikamwambia ndugu yangu mbona hakuna kitu kama hicho.

“Pamoja na kulalamika hivyo, wenzake  wa vyama NCCR-Mageuzi,CUF walikuwapo, jamani hatuna haya mambo, nawaomba tena wasiendelee kupotosha umma… si si mata ya kwanza kutoa madai haya,”alisema Jaji Lubuva.

Kuhusu madai ya Mbowe kwamba kuna kura feki ambazo zimeanza kusambazwa mikoani, Jaji Lubuva alisema hakuna kitu kama hicho.

“Kila siku nawasikia wanasema wanataka kulinda kura, huku ni kutapatapa tu…sasa sikia wanasema kuira zimepelekwa mikoani hakuna kitu hiki…nasema kwa kujiamini hakipo,”alisema.

Kauli ya Jaji Lubuva, imekuja muda mfupi baada ya Mbowe ambaye pia ni mgombea ubunge Jimbo la Hai, kuibua tuhuma hizo katika mkutano wa hadhara mkoani Kilimanjaro.

Katika madai yake, Mbowe alisema wakurugenzi wote katika tume ya uchaguzi wameondolewa na kuwekwa maofisa wengine kutoka taasisi za kijeshi kwa lengo la kutaka kuhujumu uchaguzi.

Mbowe

Akihutubia mkutano wa kampeni uliofanyika kwenye Uwanja wa Himo Polisi mkoani Kilimanjaro katika Jimbo la Vunjo, Mbowe alisema mbali na kubadilisha viongozi hao, lengo ni kuiba kura na tayari Serikali imeanza kutawanya kura kwenye mikoa mbalimbali nchini.

“Mtu mwenye wajibu wa kisheria wa kusimama uchaguzi ni NEC  baada ya CCM kuona Lowassa (mgombea urais wa Chadema, Edward Lowassa),  anashinda wameamua kuandaa mazingira ya kuchakachua tume yenyewe.

“Mkurugenzi wa Uchaguzi, Malaba (Julius) walianza kumwondoa yeye mwezi mmoja uliopita wakaleta mwingine, wiki mbili zilizopita wakurugenzi wote wamewang’oa na kuwaingiza wengine wa mwisho kuondolewa alikuwa mkurugenzi wa idara ya Tehama, inayoshughulika na daftari la kudumu la wapiga kura.

“Wameanza mkakati mwingine wa kutengeneza kura bandia na tayari zimepelekwa mkoani Kilimanjaro,” alisema Mbowe.

Hata hivyo, Mbowe alisema hakuna mkakati wowote ovu utakaopangwa na CCM bila wao kuujua kwa sababu kila wanachokipanga asubuhi, wao wanakipata mchana.

Alisema mabadiliko ambayo Ukawa unayapigania, yanamgusa kila Mtanzania bila kujali dini yake wala kabila lake hivyo ni vigumu mtu kujaribu kuyahujumu.

Alisema vingozi kama mgombea ubunge Jimbo la Vunjo, James Mbatia (NCC-Mageuzi), wana mchango mkubwa na kazi ya kuendelea kufanya kwa ngazi ya taifa ili kuhakikisha mabadiliko hayo yanatokea.

“Tumekuja hapa viongozi wote kwa sababu ya kazi kubwa anayofanya Mbatia kitaifa, mabadiliko tunayozungumza si kwa faida ya yake wala Lowassa ( Edward) ni kwa faida ya Watanzania wote,” alisema Mbowe.

“Nyie ni kati ya watu  wachache mliyepata mgombea ambaye hata taifa linamhitaji, huu ni mwaka wa mabadiliko, mimi nilikuwa CCM, Lowassa na viongozi wengine wametoka ili kuleta mabadiliko, katika mfumo wa vyama vingi kama chama hakijatekeleza walichoahidi lazima kitoke madarakani,” alisema.

Msemaji wa JWTZ

Naye Msemaji wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) Kanali  Ngamela Lubinga alipoulizwa kuhusu madai hayo, alisema hayana ukweli wowote.

“Siwezi kukupa majibu siko sehemu nzuri, lakini madai haya yalishatolewa ufafanuzi na tume yenyewe kupitia Elius  Malima,”alisema Kanali Lubinga.

Lowassa naye anena

Kwa upande wake, mgombea urais wa Ukawa kupitia Chadema, Edward Lowassa alisema ameamua kuwania nafasi hiyo kwa sababu anauchukia umasikini na CCM imeshindwa kulitatua kwa miaka 50.

“Miaka 50 ya CCM ni shida, nagombea urais kwa sababu nachukia umasikini, umasikini ni ujinga, siutaki, nitaanza na eneo la elimu,” alisema.

Akiwa Kahe, Lowassa alisema endapo wananchi watashindwa kufanya mabadiliko na kurudi kwenye maisha ya zamani itakuwa tabu kubwa.

Mbatia

Kwa upande wake,mgombea ubunge wa Jimbo la Vunjo, James Mbatia (NCCR-Mageuzi) pamoja na mambo mengine alizungumzia mdahalo wa wagombea urais.

“Mdahalo wanaoutaka CCM na lowassa si saizi yake, Dk. Magufuli aje kwangu nimtoe jasho, namwambia hata kama ni leo jioni aje kwangu nimtoe jasho. Yeye ni saizi yangu si saizi ya Lowassa,” alisema.

Akiwa Kahe, Mbatia aliwataka wananchi kutumia haki yao ya kupiga kura, kwani hiyo ni haki ya kila mwenye sifa za kufanya hivyo.

“Kama una haki ya kupiga kura, uwezo wa kupiga kura, usipopiga kura, huna haki ya kulalamika,” alisema Mbatia.

Katika hatua nyingine, Mbatia aliawaambia wananchi wa Kahe kuwa wakimchagua kuwa mbunge, ndani ya siku 14 atahakikisha hospitali ya kata hiyo inapata umeme.

Alisema suala hilo halihitaji kulisemea bungeni ama kuisubiri serikali ifanye hivyo bali ni jambo la kufanywa na mbunge pekee.

Dk. Magufuli

Naye Dk. Magufuli alibeza kauli za wapinzani akisema kuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) hakiwezi kung’oka madarakani kama jino.

Dk. Magufuli alitoa kauli hiyo wakati wa mkutano wake wa kampeni wilayani Mbarali mkoani Mbeya jana.

Alisema anashangazwa na watu wanaotaka CCM ing’oke madarakani na kueleza kuwa chama hicho hakiwezi kung’oka kirahisi, kwani kina mizizi kuanzia ngazi ya kijiji.

“Eti kuna watu wanapitapita mitaani wanasema CCM imechoka, lazima ing’oke madarakani.

“Ehee  wakae wakijua CCM haiwezi kung’oka kama jino…ndivyo walivyoamua Watanzania wakae wakijua,” alisema.

Kuhusu  mgogoro wa shamba la Kapunga kati ya mwekezaji na wananchi, Dk. Magufuli ameahidi kulirudisha shamba hilo kwa wananchi iwapo atachaguliwa kuwa rais wa awamu ya tano.

Alisema suala hilo ni kipaumbele chake cha kwanza kama akishinda urais na kuingia madarakani.

Alisema anatambua namna wananchi wanavyohangaika kwa kukosa mahali pa kuendeshea shughuli za kilimo, wakati mwekezaji kwa kushirikiana na baadhi ya viongozi  wamemega ardhi ya wananchi.

Alisema katika ubinafsishaji wa shamba hilo, mwekezaji alitakiwa kupewa ekari 5,000 na badala yake amepewa ekari 7,000 kinyume cha utaratibu.

Alisema mgogoro huo umechukua muda mrefu, kwani aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Modestus Kilufi alishindwa kuwasilisha hati za mashamba hayo serikalini ili hatua stahiki zichukuliwe.

Baada ya kushindwa kura za maoni, Kilufi alijunga na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema),  ambako alikaa kwa siku tano, kisha kujiunga na Chama cha ACT-Wazalendo na kuteuliwa kugombea ubunge wa Mbarali.

Alisema hayuko tayari kuongoza nchi na kuona wananchi wake wakikosa eneo la kuendeshea kilimo kwa ajili ya masilahi ya mwekezaji.

“Natambua Igurusi na Mbarali, mmekuwa na kilio kikubwa kuhusu shamba la mpunga la Kapunga, mwekezaji badala ya kupewa ekari 5,000 amepewa zaidi ya ekari 7,000.

“Tena katika ekari hizi, zipo 1,800 ambazo ni mali ya wananchi, ninasema kama mtanichagua nitatumia sheria namba 4 ya ardhi  na sheria namba 5 ya vijiji zote za mwaka 1999, nitafuta hati za shamba hili na kurudisha kwenu wananchi.

 

“…unapokuwa rais wa nchi kwa mujibu wa sheria, ardhi yote inakuwa chini yako, nami nasema hapa nitaifuta hati hii mchana kweupe kikubwa ninawaomba mnichague,” alisema Dk. Magufuli.

Kuhusu askari wa Hifadhi ya Taifa (TANAPA) katika Bonde la Ihefu kuwapiga wananchi na kuwafukuza, Dk. Magufuli alisema suala hilo halitatokea katika uongozi wake.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles