27.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

MIMBA ZA UTOTONI TISHIO WILAYANI MPANDA

Na Walter Mguluchuma-Katavi


MIMBA za utotoni bado ni tishio kubwa  katika Manispaa ya Mpanda mkoani Katavi ambako wasichana  624 walio na umri wa chini ya miaka 18, wamejifungua   katika  vituo vya  afya  vilivyopo katika  manispaa hiyo.

Hayo yalisemwa  hapo  jana  na Mkuu wa  Mkoa wa  Katavi, Meja Jenerali  mstaafu, Raphael  Muhuga, wakati wa  uzinduzi  wa kampeni  ya  siku  16 za kupinga ukatili  wa  kijinsia   zilizofanyika  viwanja  vya Sabasaba  Kabungu  wilayani  Tanganyika.

Meja Jenerali Muhuga alisema  taarifa   kutoka  katika  vituo vya  afya  vya Manispaa ya  Mpanda  ya kipindi cha mwaka jana inaonyesha wasichana 624 wenye  umri wa chini ya  miaka 18 walijifungua  katika  vituo   vya afya vilivyopo  katika  manispaa  hiyo na kwamba kiwango hicho ni kikubwa na ni tishio.

Alisema  utafiti  wa  afya  ya uzazi  na  mtoto  na  viashiria  vya  maralia   wa mwaka   2015/16 uliofanywa  na Ofisi ya  Taifa ya Takwimu (NBS)  kwa  kushirikiana  na   Wizara  ya  Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na  Watoto umeonyesha  Mkoa wa  Katavi  unaongoza kitaifa kwa tatizo hilo.

Alisema utafiti  huo umeonyesha  kitaifa kuwa  asilimia 27 ya  wasichana  wa   miaka   15   hadi 19 wameishaanza  uzazi, huku asilimia 21 wakiwa wamezaa  mtoto hai angalau mmoja, huku  Mkoa wa   Katavi asilimia  45 ya   wasichana   wenye umri wa   miaka 15   hadi  19  tayari ni wazazi.

Kuhusu unyanyasaji wa  kijinsia, alisema kesi  1,178 ziliripotiwa  katika vituo  vya kutolea  huduma  za   afya mkoani humo na maofisa ustawi wa jamii mwaka   2016.

Alisema kati ya kesi hizo, kesi 401 zilihusu ukatili wa  kimwili , 66 zilihusu  ukatili wa  kingono, 264 zilihusu  ukatili  wa  kisaikolojia  na  447 zilihusu kutelekezwa watoto na familia zao.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya  Mpanda, Liliani Matinga,   aliwataka wanawake ambao  wana tabia ya kupiga waume zao  waache  tabia hiyo mara moja kwa kuwa inawaaibisha wanawake wote nchini.

Naye Kamanda wa Polisi wa  Mkoa  wa Katavi, Damas  Nyanda, alisema licha ya jitihada zinazochukuliwa  na  Serikali  kwa kushirikiana  na  makundi  mbalimbali  ya kijamii, takwimu  bado  zinaonyesha  ongezeko  la ukatili  wa kijinsia.

Alisema ongezeko hilo linachangiwa  na changamoto zifuatazo  ambazo ni  imani za kishirikina, mila  na desturi  za  baadhi ya makabila, umasikini,  elimu na ukosefu wa  nyumba  salama, ambapo  baadhi ya wazazi  wamekuwa wakiwalaza wageni wao na  watoto wao na kusababisha  wageni hao kuwafanyia vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles