25.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Mfumo mpya wa Usimamizi wa Watumishi wa Umma kuanza Julai

*Utaondoa matumizi ya karatasi, upendeleo

Na Ramadhan Hassan, Dodoma

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Jenista Mhagama amekutana na viongozi wa vyama vya wafanyakazi nchini ambapo amesema mfumo mpya wa Usimamizi wa Utendaji Kazi kwa Watumishi wa Umma (PEPMIS) unatarajiwa kuanza kazi Julai mwaka huu.

Amesema lengo ni ili kuondokana na kero za usimamizi wa utendaji kazi zilizojitokeza katika utekelezaji wa mfumo wa awali wa OPRAS, ambao haukuakisi hali halisi

Kauli hiyo ameitoa April 9,2022 jijini Dodoma wakati wa kikao kazi kati ya serikali na viongozi wa Vyama vya Wafanyakazi kuhusu mtazamo wa serikali ya awamu ya sita katika kuimarisha utumishi wa umma, uwajibikaji wa hiari na matumizi ya mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kwa watumishi wa umma.

Waziri Mhagama amesema kuwa ili kupata mfumo sahihi wa kupima utendaji kazi wa Watumishi wa Umma na taasisi kama ilivyoelekezwa na Rais Samia.

“Ndio maana Ofisi yangu tumepokea maelekezo ya Rais ya kuihakikisha tunaweka mifumo imara itakayotuwezesha pia kufikia mipango mbalimbali ya maendeleo kutokana na utendaji mzuri kwa watumishi wa umma,” amesema Mhagama.

Amesema mfumo mpya wa Usimamizi wa Utendaji Kazi kwa Watumishi wa Umma (PEPMIS) unatarajiwa kuanza kazi Mwezi Julai mwaka huu ili kuondokana na kero za usimamizi wa utendaji kazi zilizojitokeza katika utekelezaji wa mfumo wa awali wa OPRAS, ambao haukuakisi hali halisi ya utendaji kazi wa watumishi hali iliyoleta hisia za kupendeleana au kuoneana.

“Mfumo mpya wa PEPMIS utakuwa ni wa kielektroniki na utaondokana na matumizi ya makaratasi, pia utaongeza uwazi katika usimamizi wa watumishi na kuondoa upendeleo na uonevu katika upimaji wa utendaji wa watumishi,pia mfumo huu pia utahamasisha uwajibikaji wa hiari na kurahisisha upatikanaji wa taarifa za utendaji kazi wa watumishi,”amesema Waziri Mhagama.

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Jenista Mhagama.

Aidha, amesema kuwa Ofisi yake imeendelea kuimarisha utekelezaji wa Sera ya Serikali Mtandao na kujenga mifumo ya TEHAMA inayohusu uendeshaji wa Serikali wa kila siku na kurahisisha utoaji wa huduma bora kwa umma.

Mhagama amesema, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma imefanikiwa kujenga Mfumo wa Sema na Waziri , Mfumo wa e-mrejsho, Mfumo wa Dawati la Huduma kwa Mteja maarufu kama UTUMISHI Call Centre, mfumo maalum wa Tathmini ya hali ya Mfumo wa Huduma Mtandao kwa Watumishi (Watumishi Portal).

Kwa upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu) Joyce Ndalichako amesema kuwa pamoja na juhudi za serikali za kupima utendaji kazi serikalini Rais amelekeza ushirikishwaji wa Vyama vya Wafanyakazi ili waendelee kuwa daraja kati ya waajiri na Wafanyakazi kwa kuchochea na kuhimiza utamaduni kwa Wafanyakazi kudai haki na kutimiza wajibu wao.

Ameongeza kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu- Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu imeendelea kutekeleza maagizo ya Rais kwa kukamilisha Mfumo wa Kielektroniki wa utoaji wa Vibali vya Kazi kwa raia wa kigeni ambao umepunguza muda wa kushughulikia maombi ya vibali vya kazi kutoka siku za kazi 14 hadi siku 7.

Naye Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Nchini (CWT), Deus Seif ameishukuru serikali kwa kuja na mfumo huo mpya ambao utasaidia kwa kiasi kikubwa kumaliza changamoto kwa watumishi wa umma.

“Mfumo wa awali wa OPRAS uligubikwa na malalamiko mengi kwa kuwa ulikuwa hautendi haki kwa watumishi katika kupatiwa stahiki na masuala mbalimbali ikiwemo hatua zinazochukuliwa kwa mtumishi pale anapokuwa amekiuka maadili ya utumishi,” amesema Mhagama.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles