26.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Maswali magumu sakata la Messi, Simba

messi1NA ABDUCADO EMMANUEL, DAR ES SALAAM
SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF), tayari limemaliza mgogoro wa mkataba uliokuwa ukimhusisha winga, Ramadhan Singano ‘Messi’ na uongozi wa klabu yake ya Simba.
Messi alikuwa akidai mkataba wake umechezewa na Simba kwani awali ulitakiwa kumalizika Julai mwaka huu, lakini uliopo kwa uongozi hivi sasa unaonyesha unamalizika Julai mwakani.
Hivyo katika kikao walichokiandaa TFF juzi kuzikutanisha pande hizo mbili, umetoka uamuzi wa kufuta mikataba yote na sasa wametakiwa kuingia makubaliano mapya kwa ajili ya msimu ujao wa 2015/2016.
Kwenye kikao hicho upande wa Simba uliwakilishwa na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji, Collin Frisch, Messi yeye alikuwa pamoja na Mwenyekiti wa Chama cha Wanasoka Tanzania (Sputanza), Mussa Kissoky aliyekuwa akimtetea.
Upande wa TFF alikuwepo Katibu Mkuu wa Shirikisho hilo, Celestine Mwesigwa, aliyekuwa akizihoji pande zote mbili kwenye kikao hicho kilichochukua takribani saa mbili (kuanzia saa 6 hadi 8 mchana).
Messi hakuupokea vizuri uamuzi huo kwa kudai kuwa: “Wamesema tukae chini tufanye makubaliano mapya, mikataba yote haipo, lakini kisheria mimi niko huru, bado sijajua kama tukishindwa kuelewana na Simba itakuaje, namuachia Mungu.”
Mara baada ya uamuzi huo wa TFF, yapo maswali magumu ya kujiuliza kutokana na utata ulioghubika suala hilo na namna lilivyomalizwa, baadhi ya hayo ni:

Nani aliyefoji mkataba?
TFF imeamua kulimaliza suala hili kwa staili ya kufunika kombe ili mwanaharamu apite, lakini bado haijaweza kutaja ukweli nani alikuwa ana haki kwenye hilo.
Uamuzi wa TFF bado haujawaingia akilini wadau wa soka, kwani hawajaeleza nani amefoji mkataba huo kati ya Messi au Simba.

TFF inaogopa nini kumtaja aliyefoji?
Hata kama ni Messi ndiye amefoji mkataba aliokuwa nao au Simba imefanya hivyo, kwanini TFF inaogopa kumtaja aliyehusika au inamlinda mtu na kukubali kukumbatia uozo kwenye soka letu?

Katibu TFF alikuwa na uhalali kuwahoji?
Tumeona mambo mbalimbali ya usajili na mikataba ya wachezaji ndani ya TFF yanapitiwa na Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji ya Shirikisho hilo.
Hili suala la Messi linalohusisha mambo ya kisheria, limekuwa tofauti sana kwani hatujaona chombo hicho kikihusishwa badala yake Katibu wa TFF, Mwesigwa ndiye aliyelimaliza, lipo la kujiuliza je, ilikuwa ni halali kwa bosi huyo kushughulikia suala hilo.

Mikataba ya wachezaji iliyoko TFF ni mapambo?
Kwa kawaida mchezaji anapoingia mkataba na timu, taratibu zinazofuata ni yeye kupewa nakala moja nyingine inabakia kwa timu na ‘copy’ moja hupelekwa TFF kama uthibitisho, huku takwimu zikiingizwa kwenye mfumo wa kielektroniki.
Kutokana na uamuzi huo wenye utata uliofanywa kwenye sakata hilo, je, inamaanisha TFF wameshindwa kufananisha mkataba wa Messi waliokuwa nao na hiyo inayolalamikiwa au mikataba waliyonayo ipo kama mapambo tu?

TFF inatunga sheria kuzikalia au kutumia?
Bado kuna maswali mengi watu wanajiuliza kama TFF inatunga sheria zake kuzikalia au kuzitumia wakati wanaamua masuala mbalimbali yanayokiukwa? Hata wale wanaofoji mikataba au nakala yoyote nao wamewekewa sheria za kuwabana.
Kwa mujibu wa Kanuni za Nidhamu za TFF toleo la mwaka 2012, Sura ya Tano inayozungumzia masuala ya kufoji, Ibara ya 61 (1, 2 na 3) inasema: “Mtu yeyote anayejihusisha na masuala ya soka atakayekutwa na hatia ya kughushi au kutengeneza nyaraka za kisheria kwa lengo za kuzitumia atafungiwa pamoja na kupigwa faini.

“Kama ni mchezaji ambaye amehusika, atakumbana na adhabu ya kufungiwa angalau kutocheza mechi sita. Kama ni kiongozi, wakala wa mchezaji au wakala wa mechi atafungiwa kutojihusisha na shughuli za mpira kwa kipindi cha miezi 12.”

Messi yupo huru au mali ya Simba?
Mikataba yote miwili inayodaiwa kuwa na utata imefutwa kwenye kikao hicho na sasa pande hizo mbili zimeambiwa ziingie makubaliano mapya.
Lakini bado haijajulikana Messi yupo kwenye aina ipi ya usajili hivi sasa, hapa namaanisha yeye bado ni mali ya Simba licha ya mikataba hiyo kufutwa au ni mchezaji huru anayeruhusiwa kufanya mazungumzo na timu nyingine yoyote?
Kama ni mali ya Simba, je, ni kwa mkataba upi? Huu ni utata mwingine iliyouanzisha TFF kama bado hawajaujua.

Kwanini Simba tu masuala haya?
Sakata hili la Messi si la kwanza kutokea kwenye klabu hiyo, msimu wa 2007/2008, kiungo Athuman Idd ‘Chuji’ naye aliingia kwenye mzozo kama huu na Simba baada ya kumaliza mkataba na kujiunga kwa mahasimu wao Yanga.
Simba ilimng’ang’ania Chuji ikidai bado ina mkataba naye, lakini mkataba aliokuwa nao Chuji ulionyesha umemalizika, jambo hilo lilimuathiri kiungo huyo kwa kukaa nje ya dimba nusu msimu na suala hilo lilipelekwa kwenye vyombo vya dola na kumalizwa kimya kimya. Je, kwanini mambo haya yanajirudia Simba?

Mchezaji gani anafuata baada ya Messi?
Udhaifu wa TFF kushindwa kuyaamua masuala haya ya utata kwenye usajili ambayo yanajirudia kila kukicha, imepelekea wahusika wa mambo hayo kuendelea kuyafanya kila siku unapofika wakati wa usajili.
Kutokana na historia ya masuala hayo kujirudia, lipo la kujiuliza kwenye hilo, je, ni mchezaji gani anayefuata kufanyiwa hilo tena baada ya hili la Messi kumalizwa kienyeji?

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles