27.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Marekani yakata misaada Tanzania

mtz1*Yachukizwa na Uchaguzi wa marudio Zanzibar

NA FLORIAN MASINDE, DAR ES SALAAM

SERIKALI ya Marekani kupitia Shirika lake la Changamoto za Milenia (MCC), imesitisha kuipatia Tanzania msaada wa Dola milioni 472.8 za Marekani, ambazo ni sawa na takriban Sh trilion moja kwa ajili ya miradi ya maendeleo kupitia awamu ya pili ya mkataba wa shirika hilo.

Hatua hiyo imetokana na Serikali ya Tanzania kushindwa kutoa maelezo ya kuridhisha kuhusu kufutwa kwa matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar uliofanyika Oktoba 25, mwaka jana.

Mbali na hilo, MCC pia ilihitaji kupata uthibitisho kutoka kwa Serikali ya Tanzania kuhusu Sheria ya Makosa ya Mtandao kutumika kukwaza uhuru wa kujieleza na kuwakamata watu wakati wa mchakato wa uchaguzi.

Uamuzi huo umekazia taarifa ya awali iliyotolewa Desemba 16, mwaka jana na Serikali ya Marekani kupitia shirika hilo, ambapo ilitangaza kusitisha msaada wa dola milioni 472.8 ambazo ni sawa na Sh trilion moja.

Tamko la MCC

Uamuzi huo ni wazi kuwa umeigharibu Serikali ya Tanzania kwa kukosa wastani wa Sh trilioni moja za miradi ya maendeleo, baada ya MCC kuamua kutoshirikiana na Tanzania.

Tamko hilo la MCC kuhusu uamuzi wa Bodi ya Wakurugenzi kusitisha ubia na Tanzania, lilitolewa jana jijini Dar es Salaam na Balozi wa Marekani, Mark Childress.

Mara kwa mara na Serikali ya Marekani na Jumuiya ya Kimataifa zilihoji kuhusu uchaguzi wa marudio wa Machi 20, mwaka huu ambao walidai kuwa haukuwa jumuishi na wenye uwakilishi stahiki.

“Serikali ya Tanzania haijachukua hatua stahiki kuhakikisha kuwa uhuru wa kujieleza na kujumuika unalindwa katika utekelezaji wa Sheria ya Makosa ya Mtandao.

“Mojawapo kati ya vigezo vya msingi kabisa ambavyo MCC hutumia kuingia ubia na nchi yoyote, ni dhamira ya dhati ya nchi hiyo kuimarisha demokrasia na kuendesha chaguzi zilizo huru na za haki.

“….uchaguzi visiwani Zanzibar na matumizi ya Sheria ya Mtandao yanakwenda kinyume kabisa na dhamira hii.  Kwa sababu hiyo, wakati ambapo Marekani na Tanzania wanaendelea kuchangia vipaumbele vingi, Bodi ya Wakurugenzi ya MCC imeona kwamba Serikali ya Tanzania imekuwa ikichukua hatua zisizoshabihiana na vigezo vya kupata sifa ya kuingia ubia na MCC,” ilieleza taarifa hiyo.

Kutokana na uamuzi huo, Tanzania inaweza kuathirika katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo ikiwamo sekta ya miundombinu kama vile umeme, barabara na maji.

Katika awamu ya kwanza ya fedha za MCC, Tanzania ilipata dola za Marekani milioni 698 (sawa na Sh trilioni 1.46) ambazo zilitumika kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya barabara.

Barabara zilizojengwa kupitia fedha hizo za awamu ya kwanza ni Tunduma- Sumbawanga, Tanga-Horohoro na Namtumbo- Songea- Mbinga.

Desemba 10,  mwaka juzi Marekani pia ilibainisha hatua ya uamuzi wa utolewaji wa fedha za awamu pili za MCC kwamba utategemea  hatua zitakazochukuliwa na Serikali ya Tanzania kuhusu sakata la uchotwaji wa fedha zaidi ya Sh bilioni 200 katika akaunti ya Tegeta Escrow.

Kauli ya Serikali

Akizungumzia uamuzi huo, Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Balozi Dk. Augustine Mahiga, alisema uamuzi huo utawaumiza Watanzania.

Alisema kutokana na hali hiyo bajeti ya mwaka 2016/2017, itaathirika kutokana na uamuzi huo wa MCC kwa Tanzania.

Balozi Mahiga alikiri kuwa uamuzi wa Bodi ya MCC utaathiri bajeti ijayo ya serikali, kwa kuwa fedha hizo ambazo zingetolewa kwa kipindi cha miaka mitano zingetumika katika miradi ya nishati ya umeme vijijini.

Alisema Januari mwaka huu MCC ilitoa taarifa kuwa misaada ya kawaida inayotolewa kwa ajili ya elimu na afya ambayo ni Sh milioni 700 itaendelea kutolewa kama kawaida kila mwaka.

Alisema kawaida fedha hizo hutolewa kwa nchi iliyotimiza vigezo vilivyowekwa na Serikali ya Marekani ambavyo ni utawala bora, uchaguzi huru na haki pamoja na demokrasia isiyo na shaka.

“Hivyo vyote Tanzania imekuwa ikisifika lakini kwa sababu hii iliyotolewa na Bodi ya MCC kuwa Uchaguzi wa Zanzibar haukuwa huru na haki na demokrasia haikufuatwa si za  kweli, kwani Tanzania inazingatia masuala hayo kwa mstakabali wa maendeleo ya Taifa.

“Uamuzi wa Washington tutaadhibiwa wote, Muha wa Kigoma na Mpemba wa Pemba wote tutaumia. Huo ni uamuzi wao hatuwezi kuingilia, lakini na yetu hatutaki yaingiliwe.

“Kwa suala la Zanzibar tumejitahidi kueleza pamoja na kuchukua hatua ya kuimarisha demokrasia na tutaendelea kufanya hivyo,”alisema Balozi Mahiga.

Wadau wanena

Baadhi ya watu mbalimbali wakiwamo wanasiasa wamejadili uamuzi wa Bodi ya MCC, huku wakisema kuwa hatua hiyo ni matokeo ya ubabe wa Serikali.

Kwa upande wake Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe (ACT-Wazalendo), alisema uzalendo ni kutaka haki ya kidemokrasia Zanzibar.

“Sitakubali kuvishwa koti la uzalendo kwenye suala la MCC. Hilo ni suala la CCM, kukosa misaada ya Marekani ni matokeo ya ubabe wa CCM kuhusu Zanzibar.

“Haina mahusiano yoyote na uhuru wa nchi yangu, nawasihi Wazanzibari wawe na subira Mola kamwe hatawatupa, haki itapatikana tu. Nawasihi Watanzania kuelewa kwamba CCM ndio imetufikisha hapa na iubebe mzigo huu bila kufanya ni mzigo wa nchi,” alisema Zitto.

Chama cha ACT-Wazalendo, kimetoa tamko na kusema kuwa kimepokea kwa masikitiko uamuzi wa Bodi ya Wakurugenzi wa MCC wa kusisitisha uhusiano na Tanzania.

Makamu Mwenyekiti, Kamati ya Katiba, Sheria na Mambo ya Nje, Theopister Kumwenda, alisema tangu kuanzishwa kwa MCC kumesaidia miradi mingi ya maendeleo nchini ikiwemo ujenzi wa barabarani na usambazaji wa umeme vijijini.

Mtatiro

Naye aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa CUF (Bara), Julius Mtatiro, alisema Tanzania imenyimwa fedha hizo na watakaoumia ni wananchi.

“Tumenyimwa fedha hizi na watakaoumia ni wananchi. Kwa hiyo dhambi ya CCM inalipwa na Watanzania wote na kisha viongozi wa CCM wanaanza kutuhubiria uzalendo.

“Waliopora haki Wazanzibari kwenye masanduku ya kura, eti pia ulikuwa ni uzalendo,” alisema Mtatiro.

Alisema pamoja na hali hiyo wapo watu wanaoibuka na hoja ya umuhimu wa kutolilia misaada ya wazungu ambao pia wanatakiwa kujiuliza kwani misaada ya MCC aliyekwenda kuiomba ni nani.

“Mnapoanzisha hoja ya taifa kujitegemea kiuchumi na kumnukuu Mwalimu Nyerere, Nkrumah n.k. Tunawauliza swali jingine, ni nani amekuwa na mamlaka ya kulifanya taifa lijitegemee kiuchumi kwa miaka 50 iliyopita? Si ni nyie nyie?

“…na tena hamtaki kusaidiwa na mawazo mapya hata baada ya kushindwa na kuendelea kuwalamba miguu wahisani,” alisema.

Magufuli na wahisani

Septemba 29, mwaka jana wakati wa kampeni Rais Dk. John Magufuli, aliwashangaa watu wanaokejeli safari za nje za Rais mstaafu wa awamu ya nne, Jakaya Kikwete na kusema kwamba manufaa ya ziara hizo ni makubwa kuliko wanavyofikiri.

Alisema kupitia safari hizo, Rais Kikwete amefanikiwa kuwashawishi wafadhili kutoa misaada ya miradi mbalimbali nchini.

Dk. Magufuli alitoa mfano wa Sh bilioni 992 zilizotolewa na Serikali ya Marekani hivi karibuni kupitia mfuko wa MCC kwa ajili ya miradi ya umeme kama sehemu ya matunda ya safari za Rais Kikwete nchi za nje.

“Mabilioni yaliyotolewa na MCC, yatasaidia kusambaza umeme katika mikoa na vijiji vingi nchini na tayari mipango imekamilika ya kuwafikishia wananchi nishati hiyo,” alisema Rais Magufuli.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles