Na Mwandishi Wetu, Chato
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, amesema Mama Mzazi wa Hayati Rais Dk.John Magufuli bado ni mgonjwa na yupo kitandani kwa miaka miwili sasa na Serikali itahakikisha madaktari wanamtibu hadi atakaporejea katika hali yake ya kawaida.
Akizungumza leo Ijumaa Machi 26, wilayani Chato mkoani Geita wakati wa Ibada ya mazishi ya aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano, Hayati Dk. Magufuli, Majaliwa amesema hadi sasa Mama Mzazi wa Hayati Rais Magufuli yupo kitandani akiendelea na matibabu.
“Nimeongea na Rais kuhusiana na jambo hili na tutahakikisha madaktari wanamtibu bibi yetu hadi pale atakaporejea katika hali yake ya kawaida,” amesema Majaliwa.
Waziri Majaliwa amesema msiba huo umewagusa Watanzania wengi na kama Taifa hawana budi kumshukuru Mungu na kumuenzi Hayati JPM kwa vitendo.
Pia amewashukuru Wasanii, Waandishi wa Habari na Watanzania kwa ushirikiano wanaoonesha katika kipindi chote cha maombolezo.