Brighiter Masaki -Dar es salaam
MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, amewataka wananchi wa mkoa huo kutojifanya wajuaji kwenye jambo la kutangaza ugonjwa wa corona.
Akizungumza na waandishi wa habari jana alisema watu wa mkoa wake ndio wanaongoza kwa kujifanya wajuaji na kutoa taarifa za wagonjwa wakati sio jambo sahii.
“Sasa niwaombe msilete ujuwaji kwenye janga hili la corona tujifanye wajinga kidogo”
“Mwananchi hauna mamlaka ya kutangaza mtu mwenye corona … wenye mamlaka anayo Waziri wa Afya, Waziri Mkuu na Rais, hata mimi hamjanisikia nikitangaza kwenye mkoa wangu kuna wagonjwa wangapi?”alisema Makonda
Pia alisema kuwa watu wanatakiwa kuwa watulivu ili Mungu afanye miujiza yake.
“Tunaweza kula na kusherekea Pasaka bila corona hili litapita kama matatizo mengine yalivyopita.”
“Naomba tusifanye jambo la kunyanyapaa watu wenye corona na tusitumie mitandao ya kijamii kuwajaza hofu.”
“Sio unamwona mtu hospitali unaanza kutangaza kuwa anaumwa corona magonjwa yapo mengi, corona haijasitisha magonjwa mengine mtu anaweza kwenda hospitali kwa magonjwa mengine”alisema Makonda
Aidha amewataka watu kuacha kwenda sehemu za starehe na kwamba wakitaka kunywa wafanye hivyo majumbani kwao na familia zao.
“Wanaopenda kwenda Club na Leo (jana) ni Ijumaa, fungua muziki nyumbani kwako cheza na familia yako, na wanaoenda baa kunywa agiza kinywaji nyumbani kwako, na ukikuta basi la mwendokasi limejaa shuka uoga ndio akili usijifanye mjuaji itakukosti”
“Kwa upande wangu nimewasiliana na ndugu zetu wa China kupitia Balozi wamekubali kuleta vifaa vya kupimia Corona Dar es Salaam muda sio marefu vinakuja” alisema Makonda
Alisisitiza kuwa wenyeviti wa serikali ya mitaa wanatakiwa kuwatambua watu walioko mtaani na endapo atagundulika mgonjwa wasimfiche na wasisite kutoa taarifa ili aweze kupewa matibabu ya haraka.