33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

MAJIPU 36 YAIVA

Pg 1Na Veronica Romwald, Dar es Salaam

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (Takukuru) imetangaza inashughulikia kesi kubwa 36   zinazowahusisha watuhumiwa wenye ushawishi na hadhi kubwa nchini.

Kutokana na hali hiyo, taasisi hiyo imesema  tayari imeomba kibali cha Mkurugenzi wa Mashtaka  (DPP), ili watuhumiwa hao wanaohusisha na ufisadi mkubwa wafikishwe mahakamani kwa mujibu wa sheria.

Akizungumza na waandishi wa habari   Dar es Salaam jana, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Valentino Mlowola,   alisema tayari kuna kesi nne ambazo zimekuwa zikizungumzwa na wananchi.

Mlowola alisema  katu taasisi yake haipo kwa ajili ya kulinda wabadhirifu wa mali za umma.

Alisema kati ya hizo ipo Kampuni ya Mafuta ya Lake Oil ambayo inaelezwa kuwa ilifanya udanganyifu na kukwepa   kodi kwa kuuza kwenye soko la ndani   lita 17,461,111.58 za petroli

Kampuni hiyo inadaiwa   ilidanganya kwamba ilikuwa imesafirisha   petroli hiyo kwenda  Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kupitia Zambia, na kuisababishia  Serikali hasara ya takribani Sh bilioni 8.5.

“Takukuru imekamilisha uchunguzi wa shauri hili na mtuhumiwa na washirika wake wamepewa miezi miwili kuzirejesha mikononi mwa umma fedha zote Sh bilioni 8.5.

“Serikali ilipata hasara ya fedha hizo  kutokana na ukwepaji   kodi huo na tunajiandaa kuwafikisha mahakamni endapo watashindwa kutekeleza,” alisema Mlowola.

EGMA NA UTAKATISHAJI FEDHA

Kaimu Mkurugenzi huyo wa Takukuru, pia alizungumzia suala la hati fungani hasa kuhusu  suala la malipo ya dola milioni milioni sita (Sh bilioni 12) zilizolipwa kwa Kampuni ya Enterprise Growth Market Advisors (EGMA).

Alisema Takukuru  imebaini fedha hizo zilitakatishwa na watumishi wa umma wasio waaminifu kwa kushirikiana na baadhi  kutoka sekta binafsi wakati wakifahamu fedha hizo walizipata kwa njia haramu.

“Tupo kwenye hatua nzuri kukamilisha uchunguzi huu na watuhumiwa wote bila kujali hadhi au nafasi ya mtu pamoja na taasisi zilizohusika, tutawafikisha mahakamani kwa mujibu wa sheria,” alisema.

Tamko hilo la Takukuru limetolewa  siku chache baada ya Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango, kutangaza   Januari 17 mwaka huu kuichukuliwa hatua Benki ya Stanbic Tanzania na kutakiwa kulipa faini ya Sh bilioni tatu kwa kuhusika kufanya malipo kwa kampuni ya EGMA kinyume cha sheria.

Habari zinasema  vigogo  hao tayari wamekwisha kuhojiwa na vyombo vya dola Desemba mwaka jana kutokana na tuhuma hizo za ufisadi.

Wakati huo, Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Philip Mpango, alisema baada ya uchunguzi iligundulika ulikuwapo  upungufu kwa benki ya Stanbic Tanzania katika kufanya miamala iliyoihusisha EGMA na haikuweka utaratibu wa madhubuti wa udhibiti kuhusiana wizi wa ndani.

“Sheria inaitaka Benki ya Stanbic kutoa utetezi katika kipindi cha siku 20 ambacho kitaishia Januari 30 mwaka huu na endapo Benki Kuu haitaridhika na utetezi, benki ya Stanbic italazimika kulipa faini hiyo,” alisema Dk. Mpango ambaye kwenye mkutano huo alifuatana  na Naibu Gavana, Lila Mkila.

MWENENDO WA KESI

Mwenendo wa kesi kuhusu suala hilo iliyotolewa hukumu Uingereza, Novemba 30 mwaka jana, unasema tangu mwaka 2011 Serikali ya Tanzania ilifanya juhudi za kupata mkopo wa miradi ya miundombinu kupitia soko la kimataifa la hati fungani bila mafanikio kutokana na kile kilichoelezwa ni kukosa vigezo.

Mwenendo huo unasema benki za Standard na Stanbic kwa pamoja zilichukua jukumu la kutafuta mkopo huo kwa Serikali ya Tanzania kupitia waziri wa fedha wa wakati huo,   Mustafa Mkulo.

“Pendekezo lilikuwa Standard na Stanbic ziwasilishe wazo la kuiwezesha Serikali kupata mkopo, na lilikuwa liwasilishwe kwa waziri wa fedha kwa sharti kwamba Standard na Stanbic kwa pamoja zipokee ada ya asilimia 1.4 kwa kuandaa na kuwezesha mkopo huo.

“Standard na Stanbic zilisema kwamba wazo lao hilo lingeuzwa kama mchakato binafsi kwa mujibu wa sheria na mwongozo wa usalama wa Marekani,” unaeleza mwenendo huo wa kesi.

Katika barua pepe ya Februari 25, 2012, Kaimu Mkuu wa Masuala ya Uwekezaji wa Stanbic, Shose Sinare, aliwafahamisha watu fulani ndani ya Standard na Stanbic, akiwamo Mkuu wa Masuala ya Kimataifa ya Madeni ya Masoko ya Mitaji wa Standard na Mkurugenzi Mtendaji wa Stanbic, kwamba wazo lao limekubaliwa na waziri wa fedha.

Kwa herufi kubwa na maandishi manene, Sinare ambaye kwenye mwenendo wote huo ametajwa kwa nafasi yake bila kugusia jina lake, alibainisha kwamba benki ingepata asilimia 1.4 kama ada ya kuwezesha mpango huu kwa Serikali ya Tanzania.

Mwenendo huo unasema kuwa Mei 2012, kabla ya wazo la mpango huo kusainiwa, Waziri wa Fedha, Mkulo aliondolewa  na nafasi yake kuchukuliwa na waziri mwingine (Dk. William Mgimwa).

“Kuanzia Mei 2012 kuelekea mwishoni mwa mwaka 2012, Standard na Stanbic zilijaribu kufufua mpango huo kupitia juhudi zilizofanywa na Sinare na Mkurugenzi Mtendaji wa Stanbic (Bashir Awale), ambao walikutana na maofisa wa Serikali nchini.

Mkuu wa Kimataifa wa Madeni ya Mitaji ya Masoko alikuwa akifahamishwa hatua kwa hatua ya maendeleo hayo na Standard, pamoja na timu ya ndani ya ushauri iliyohusika kuandaa nyaraka za mpango huo.

Juni 2012, Sinare aliwasilisha kwa ofisi ya Waziri wa Fedha  nakala ya mpango huo, ukiendelea kuonyesha Standard na Stanbic kwa pamoja kama maneneja viongozi wa mpango huo, wakitarajia kupokea ada ya asilimia 1.4 ya sehemu ya mkopo huo.

Julai 2012, Stanbic ilimuajiri mtoto wa kiume wa waziri huyo mpya wa fedha.

Agosti 29, 2012, Sinare alimwandikia barua pepe Mkuu wa Masuala ya Kimataifa ya Madeni ya Masoko ya Mitaji wa Standard, kwamba yeye na Bashir wamefikia ‘mahali pazuri’ baada ya mkutano mzuri na Waziri wa Fedha na timu yake, na kwamba kwa sasa wako katika mwelekeo mzuri wa kusaini makubaliano ya mpango huo.

Mwenendo wa kesi hiyo unasema Sinare pia alimfahamisha Mkuu wa Masuala ya Kimataifa ya Madeni ya Masoko ya Mitaji wa Standard kwamba mkutano na Waziri wa Fedha ulithibitishwa ungefanyika Septemba 18.

KESI RAHCO

Akizungumzia Shirika Hodhi la Reli (RAHCO), Mlowola alisema jana kuwa  shauri hilo linahusu ukiukwaji wa sheria na taratibu za kuwapata wazabuni kwenye ujenzi wa reli ya kisasa ya kimataifa (Standard Gauge), mchakato  unaosimamiwa na RAHCO.

Alisema   baadhi ya watuhumiwa katika kesi hiyo  wamekamatwa na kuhojiwa akiwamo raia wa Kenya aliyekuwa  mtu muhimu katika mchakato wa kumpata mzabuni, Kanji Muhando.

“Mtakumbuka kuwa Rais Magufuli alitengua uteuzi wa aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa RAHCO,  Benhadard Tito, kutokana na tuhuma mbalimbali zilizokuwa zinamkabili, tunazo kesi tunazichunguza kuhusiana na TRL.

“…tupo kwenye hatua za mwisho kukamilisha uchunguzi huu na tutawafikisha mahakamani wote watakaobainika kujihusha na vitendo vya rushwa bila kujali hadhi zao wala nyadhifa walizonazo,” alisema Mlowola.

MABEHEWA TRL

Mlowola alisema  shauri la TRL linahusu ukiukwaji wa Sheria za Ununuzi wa Umma Namba 21 ya mwaka 2004 pamoja na kanuni zake kwenye ununuzi wa mabehewa 25 ya kokoto kutoka katika Kampuni ya Hindusthan Engineering and Industries Limited.

Alisema kutokana na uchunguzi wao walioufanya tayari wamekwisha kumpelekea Mkurugenzi wa Mashtaka  (DPP),  ili kibali cha kuwafikisha mahakamani watuhumiwa wote waliobainhika kujihusisha na vitendo vya rushwa na ukiukwaji wa sheria, taratibu na kanuni za ununuzi wa umma.

Ujenzi wa reli hiyo mpya yenye urefu wa kilometa 2,561 ambayo itakuwa na kiwango cha kisasa cha ‘Standard Gauge’ unatarajiwa utakuwa mradi mkubwa kutekelezwa na Serikali ya Tanzania.

Aliyekuwa Waziri wa Uchukuzi wa Serikali ya awamu ya nne, Samuel Sitta, aliwahi kusema kuwa reli hiyo mpya itakuwa tofauti na nyingine, na yenye uwezo wa kimataifa kutokana na kuchukua mabehewa ya ghorofa ambako itaanzia Dar es Salaam hadi Kigoma.

Treni hiyo itapita katika mikoa ya Tabora, Mwanza, Isaka hadi Rusumo, Kaliua-Mpanda – Karema na Uvinza hadi Musongati nchini Burundi.

Pamoja na masuala mengine, reli hiyo itasaidia kukidhi mahitaji makubwa ya ubebaji mizigo kwenda nchi jirani za DRC, Rwanda, Burundi na Uganda lakini pia itasaidia usafirishaji wa wananchi  kwenda mikoani kwa wingi na kasi zaidi.

Ujenzi wa reli hiyo ya kisasa unatokana na uamuzi wa serikali baada ya reli iliyopo   ya kiwango cha ‘Meter Gauge’ kuwa na  uwezo   mdogo ikizingatiwa kuwa ina uwezo wa kusafirisha tani milioni tano tu  kwa mwaka  ambazo haziwezi kukabili mahitaji ya mizigo katika kanda hiyo ambayo yatafikia tani milioni 30 ifikapo 2025.

Reli hiyo mpya ya kisasa   itakapokamilika itasafirisha mizigo kutoka bandari ya Dar es Salaam hadi Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kwa  muda wa saa 12 tu.

Uzinduzi wa reli hiyo ulifanyika Juni 30  mwaka jana na Rais mstaafu wa awamu ya nne Jakaya Kikwete kwa kuweka jiwe la msingi eneo la Mpiji,   Mkoa wa Pwani ambako ndipo   ujenzi utakapoanzia.

ONYO

Mlowola alisema jana kuwa Serikali imedhamiria kukabiliana na tatizo la rushwa na ufisadi kwa nia ya dhati.

Alisema  wakati wa kampeni za uchaguzi na hata alipokuwa akizindua Bunge la 11,  Rais Dk. John Magufuli alionyesha nia ya dhati kutoka moyoni mwake kwamba atalishughulikia tatizo la rushwa na ufisadi bila kumuonea mtu huruma  na aliwaomba Watanzania wamwombee kwa Mungu.

“Alisema atatumbua majipu. Majipu kama mnavyojua hayawezi kutumbuliwa bila ya kuwapo kwa vidole, sasa sisi (Takukuru) ni vidole   na tutahakikisha tunashirikiana na Rais kulishughulikia kila jipu litakalotumbuliwa.

“Ninajua watu walikuwa wakifanya kazi kwa mazoea, kama Rais alivyosema kazi yake ni kutumbua majibu na mimi ni dole gumba na watambue kwamba ‘The game is over’(mchezo umefikia tamati).

“Kwa sababu hatutasita kuchukua hatua kali za sheria kwa yeyote atakayejiingiza kulihujumu Taifa. Wananchi wana kiu ya kupata maendeleo na tunatambua kwamba bila kukusanya kodi ni vigumu kuwaletea maendeleo hayo,” alisema Mlowola.

Mlowola aliwaonya maofisa maduhuli na watekelezaji wa jukumu la kukusanya kodi kuhakikisha wanajiepusha na vitendo vya rushwa na ufisadi kwa sababu Takukuru  haitasita kuwashughulikia.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles