23.3 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Majambazi 63 mbaroni Dar

sirooAsifiwe George na Secilia Alex (A3), Dar es Salaam

JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, limewakamata watu 63 wanaotuhumiwa kujihusisha na vitendo vya unyang’anyi wa kutumia silaha katika maeneo mbalimbali ya Jiji.

Sambamba na watuhumiwa hao, pia limekamata bunduki sita za kivita, risasi 29 na magari manne ambayo yaliibiwa na kubadilishwa namba.

Akizungumza na waandishi wa habari jana ofisini kwake Dar es Salaam, Kamanda wa Polisi, Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Simoni Sirro, alisema watuhumiwa hao walikamatwa katika operesheni maalumu iliyofanyika kwa muda wa wiki moja.

Kamanda Sirro aliwataja watuhumiwa sita wa ujambazi wa kutumiwa silaha kuwa ni Ibrahim Juma (31), Samweli Mbonea (40), Anthony Kanyenye (60) wote wakazi wa Kiwalani, Shafii Ngoa (43), Rajabu Salumu (63) Joseph Gasper (34) wakazi wa Vingunguti.

Alisema watuhumiwa hao wamekiri kushiriki vitendo vya unyang’anyi wa kutumia silaha katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Dar es Salaam yakiwemo yale yaliyotekelezwa katika Hoteli ya Riki Hill na kituo cha mafuta cha Lake Oil kilichopo Buguruni.

Kamanda Sirro alisema Aprili 6, mwaka huu saa 5:00 asubuhi kikosi cha doria cha polisi kiliwakamata majambazi saba eneo la Kimara Barafu karibu na kituo cha mafuta cha Puma na Aprili 7, polisi walipambana na majambazi katika eneo la Vingunguti, Uwanja wa Koroni ambao walizidiwa nguvu na kutupa bunduki aina ya SMG iliyokatwa kitako na mtutu huku ikiwa na risasi 10 kisha wakakimbilia Bonde la Mto Msimbazi.

Alilitaja tukio lingine lililotokea Aprili 4, mwaka huu saa 8:45 asubuhi katika barabara ya Ally Bin Said, huko Masaki polisi walikamata bunduki mbili  aina ya Rifle ambazo hazikuwa na risasi.

“Silaha hizo zilionekana zikiwa zimefichwa kwa kufunikwa kwa taulo zilizokuwa na maandishi ya Collessium Fitness Club, moja ikiwa na namba A 6777013 iliyosajiliwa nchini kwa namba TZCAR 58596 na nyingine ikiwa na namba L 691848176 iliyosajiliwa kwa namba TZCAR 75062.

“Aprili 3, eneo la Mponda Mchikichini Mbagala, askari walikamata silaha moja aina ya Shortgun ikiwa na risasi nne baada ya kupata taarifa kutoka kwa wasamaria wema kuwa kuna watu wamepanga kufanya unyang’anyi wa kutumia silaha katika eneo hilo.

Kamanda Sirro alisema siku hiyo hiyo ya Aprili 4, saa 12:45 katika eneo la Mikocheni kwa Warioba polisi walimkamata Mamboleo Wiliam (41) akiwa na risasi 15 za bastola zilizokuwa kwenye magazine na alipohojiwa alikiri kufanya biashara ya kuuza risasi lakini hakusema alikozipata.

Aidha, Kamanda Sirro alisema Aprili 7 katika eneo la Bunju, polisi waliwakamata watu wakiwa na magari matatu ya wizi aliyoyataja kuwa yote ni aina ya Toyota Noah.

Uchunguzi wa awali wa polisi umeonyesha kuwa magari hayo yaliibiwa Dar es Salaama kabla ya kubadilishwa namba zake za usajili.

Alisema gari lenye namba T 924 DEM lilibainika kubadilishwa kutoka namba zake halisi ambazo ni T 814 DES, nyingine ni T924 DEM ambayo ilibadilishwa na kuwa na namba T348 DFW na gari namba T 364 DEA ambayo namba zake halisi ni T 924 DEM.

Aliwataja watu hao kuwa ni Patrick Philip (29) mkazi wa Bunju ‘B’ na Benard Charles (46) mkazi wa Sinza na kwamba katika mahojiano watuhumiwa wote walikiri kuhusika na wizi wa magari na uchunguzi unafanyika ili kubaini mtandao mzima wa wezi wa magari.

Tukio jingine lililotajwa na Kamanda Sirro ni la Aprili 6 ambapo polisi waliwakamata watu wawili wakiwa na gari moja aina ya IST nyeusi yenye namba T 750 BLZ ambayo iliibiwa eneo la maegesho ya magari Kimara Bunyokwa.

Aliwataja watu hao kuwa ni Shabani Rashidi (20) mkazi wa Kijitonyama na Issa Said (20) mkazi wa Mbagala ambao walikiri kuiba gari hilo lililotambuliwa kuwa ni mali ya Regina Lazaro(20) mkazi wa Kimara.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles