25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Magufuli amng’oa Dau NSSF

dk.magufuli*Ampeleka ubalozi, wamo Dk. Migiro, Chikawe

*Ateua makamishna polisi, pengo la NIDA lajazwa

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

RAIS Dk. John Magufuli, amemng’oa Mkurugenzi wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Dk. Ramadhan Dau na kumteua kuwa balozi.

Dk. Dau, ambaye ameiongoza NSSF kwa miaka 19, ambapo aliteuliwa mwaka 1997 na Rais mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamin Mkapa kwa vipindi viwili na baadaye akateuliwa tena na Rais Kikwete na kuhudumu katika nafasi hiyo hadi jana alipoteuliuwa kuwa balozi.

Mbali na Dk. Dau wengine walioteuliwa kuwa mabalozi katika Wizara ya Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa ambao ni mawaziri wa Serikali ya awamu ya nne Mathias Chikawe ambaye alikuwa akiongoza Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na Dk. Asha-Rose Migiro aliyekuwa akiongoza Wizara ya Katiba na Sheria.

Mbali na uteuzi huo Rais Magufuli pia amefanya uteuzi wa makamishna wanne wa Jeshi la Polisi na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya vitambulisho vya Taifa (NIDA).

Taarifa ya iliyotolewa jana na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais Ikulu na Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, Gerson Msigwa, alisema Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue,  ilieleza mabalozi hao wateule  vituo vyao vituo vya kazi kwa mabalozi hao vitajulikana baada ya taratibu husika za kidiplomasia kukamilika.

Makamishna wapya Polisi

Kwa upande wa Makamishna wa Polisi, Balozi Sefue amewataja walioteuliwa kuwa ni Naibu Kamishna wa Polisi Simon Sirro ambaye amepandishwa cheo kuwa Kamishna wa Polisi, na ameteuliwa kuwa Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam.

Kamishna Sirro anajaza nafasi iliyoachwa wazi na Kamishna Mstaafu Suleiman Kova.

Naibu Kamishna wa Polisi Albert Nyamuhanga ambaye amepandishwa cheo kuwa Kamishna wa Polisi na ameteuliwa kuongoza Idara ya Fedha, Utawala na Lojistiki ambapo ameteuliwa kujaza nafasi iliyoachwa wazi na Kamishna wa Polisi Clodwing Mtweve aliyeteuliwa kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza.

“Naibu Kamishna wa Polisi, Robert Boaz amepandishwa cheo kuwa Kamishna wa Polisi na ameteuliwa kuongoza Idara ya Intelijensia.

“Kamishna Boaz anajaza nafasi iliyoachwa wazi na Kamishna Valentino Mlowola aliyeteuliwa kuwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU),” ilieleza taarifa hiyo

Mwingine alipandishwa cheo na Rais Magufuli ni Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi,  Nsato Mssanzya ambaye amepandishwa cheo kuwa Kamishna wa Polisi na ameteuliwa kuongoza Idara ya Mafunzo na Operesheni.

Kamishna Mssanzya anajaza nafasi iliyoachwa wazi na Kamishna wa Polisi, Paul Chagonja aliyeteuliwa kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Katavi

Uteuzi NIDA

Rais Magufuli amemteua Dk. Modestus Kipilimba kuwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA).

Kabla ya Uteuzi huu Dk. Kipilimba alikuwa Mkurugenzi wa Menejimenti ya Udhibiti Benki Kuu ya Tanzania (BoT), ambapo anakwenda kujaza nafasi iliyoachwa wazi na Dikson Maimu ambaye uteuzi wake ulitenguliwa.

Januari 26, mwaka huu Rais Magufuli alitangaza kumsimamisha kazi ili kupisha uchunguzi dhidi yake Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), Dickson Maimu.

Maimu alisimamishwa pamoja na maofisa wengine wanne wa NIDA kwa tuhuma za ubadhirifu wa fedha za serikali.

Maofisa hao ni Mkurugenzi wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano Joseph Makani, Ofisa Ugavi Mkuu Rahel Mapande, Mkurugenzi wa Sheria Sabrina Nyoni na Ofisa Usafirishaji George Ntalima.

Balozi Sefue alisema taarifa zilizomfikia Rais zilionesha kuwa NIDA hadi wakati huo ilikuwa imetumia Sh. bilioni 179.6 kiasi ambacho ni kikubwa.

Alisema Rais angependa ufanyike uchunguzi na ukaguzi jinsi fedha hizi zilivyotumika, maana Rais amekuwa akipokea malalamiko ya wananchi kuhusiana na kasi ndogo ya utoaji wa Vitambulisho vya Taifa.

Rais pia ameelekeza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali afanye ukaguzi maalum wa hesabu za NIDA, ikiwemo ukaguzi wa “value for money” baada ya kuthibitisha idadi halisi ya vitambulisho vilivyotolewa hadi sasa.

Pia aliitaka TAKUKURU ifanye uchunguzi kujiridhisha kama kulikuwa na vitendo vya rushwa au la.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles