CENTAL -Hong Kong
POLISI jana walilazimika kutumia risasi za mpira na mabomu ya machozi kutawanya waandamanaji wa Hong Kong ambao hasira yao dhidi ya mpango wa serikali kuruhusu raia wa eneo hilo kupelekwa China kushitakiwa iligeuka na kuwa vurugu.
Waandamanaji hao ambao awali waliandamana Jumapili na kuahidi kurudi tena mtaani jana walizuia barabara muhimu zinazozungukwa na majengo ya Serikali huku wakiwarushia polisi mawe na vitu vingine vya hatari.
Polisi walisema walikuwa hawana jinsi zaidi ya kutumia silaha kudhibiti waandamanaji ambao walikuwa wanaelekea kuwazidi nguvu.
Serikali bado imeshikilia msimamo wake ule ule wa kutaka muswada huo upitishwe na kuwa sheria na kura ya mwisho inatarajiwa kufanyika Juni 20.
Hata hivyo Baraza la Watunga Sheria (LegCo) jana lilichelewesha muswada huo kusomwa kwa mara ya pili.
LegCo ilieleza katika taarifa yake kuwa mkutano uliopangwa kufanyika jana uliahirishwa na haijulikani ni lini muswada huo utasomwa kwa mara ya pili.
Waandamanaji wanasema hawako tayari kuondoka nje ya viunga vya Bunge hadi pale muswada huo utakapoondolewa.
Watu 22 wamejeruhiwa hadi sasa katika mapambano hayo lakini hakuna anayetajwa kuwa katika hali mbaya.
Jumatatu wiki hii siku moja baada ya kuzuka maandamano makubwa, kiongozi wa Hong Kong, Carrie Lam alisema hawezi kuvunja mpango wa serikali kuruhusu raia kupelekwa China kushitakiwa.
Lam alikuwa akijibu kile kilichodaiwa na mamia kwa maelfu ya wakaazi wa Hong Kong kumefanya maandamano mjini humo Jumapili kuupinga mpango huo wa serikali utakaoruhusu watuhumiwa kupelekwa China kukabiliwa na mashtaka.
Waandamanaji hao wanahofia itaruhusu China kuwalenga wapinzani wao wa kisiasa walioko Hong Kong.
Pamoja na hayo, kiongozi huyo alisisitiza kuwa sheria hiyo ilikuwa ni muhimu na kwamba haki zote za binadamu zimelindwa.
Chombo cha habari cha serikali ya China kimeeleza kuwa maandamano hayo ya Hong Kong yametiwa nguvu na mataifa ya kigeni.
Waandaaji wa maandamano hayo walikadiria watu milioni moja kuwa waliandamana Jumapili, ingawa polisi walisema walikuwa 240,000.
BBC lilisema kuwa iwapo kiasi cha kilichokadiliwa na waandamanaji ni sahihi, maandamano hayo yanaweza kuwa ni makubwa katika katika ardhi ya Hong Kong tangu ilipokabidhiwa kwa China na Uingereza mwaka 1997.
Katika mkutano wake na waandishi wa habari, Carrie Lam alisema sheria hiyo haitaondoa uhuru wowote ambao eneo hilo inaufurahia.
“Muswada haujawezeshwa na serikali kuu,” alisema Lam akimaanisha serikali ya China.
Alisema sheria hiyo ilipendekezwa kwa matakwa ya Hong Kong.
Maandamano