30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Lowassa: Wingi wa wagombea CCM haunitishi

lowassNa Elias Msuya
WAZIRI Mkuu mstaafu, Edward Lowassa, amesema wingi wa makada wa CCM wanaojitokeza kuchukua fomu za kugombea urais haumbabaishi, kwa kuwa ndio mchakato wa demokrasia.

Hadi sasa kuna makada 31 waliochukua fomu za kugombea urais, akiwamo Lowassa mwenyewe.

Akizungumza katika mkutano wa kuwashukuru wana CCM waliomdhamini wilayani Nzega jana, Lowassa alikitaka chama chake kutenda haki ili kupata mgombea bora.
“Kumekuwa na wagombea wengi waliojitokeza kugombea. Huu ni mchezo wa kupokezana vijiti, msiogope idadi ya wanaochukua fomu kwa kuwa ndiyo demokrasia, ilimradi haki itendeke. Tuombe Mungu haki itendeke ili tupate rais bora,” alisema Lowassa.
Aliwataka wanachama hao kujiandikisha kwenye daftari la kudumu la wapiga kura ili kumpigia kura zitakazomwezesha kuwa rais.
“Itakapofika tarehe 12 mwezi ujao, mkutano mkuu wa chama utaamua nani anafaa kushika bendera. Tuwaombee wajumbe wa mkutano mkuu wachague mtu mzuri. Kwa kanda hii ya ziwa, wallah nikipewa mambo yatakuwa vizuri,” alisema Lowassa huku akishangiliwa na wana CCM hao.
Kwa upande mwingine mjumbe wa mkutano mkuu wa chama hicho Wilaya ya Nzega, Hussein Bashe, alimhakikishia Lowassa kuwa na kura 12 katika mkutano wa CCM.
“Nakuhakikishia katika wilaya hii una kura 12 zitakazokuunga mkono kwenye mkutano mkuu… kuna kura moja tu haieleweki, lakini ikifika Julai 12 itakuwa ya uhakika,” alisema Bashe, huku akishangiliwa na umati wa wana CCM.
Bashe aliyasema hayo huku ikifahamika kuwa Mbunge wa Jimbo hilo, Dk. Khamis Kigwangalla, naye amechukua fomu ya kugombea urais kwa tiketi ya CCM.
“Kumekuwa na maneno mengi, kila siku kuna santuri inatoka, lakini nawahakikishia kuwa Lowassa yuko imara. Tumwombee tu ashinde,” aliongeza Bashe.
Akimzungumzia Bashe, Lowassa aliwataka wananchi wa Nzega kumuunga mkono kwa kuwa ndiye msaidizi wake wa karibu katika safari ya matumaini.
“Watu wamekuwa wakipita huku na huko kutafuta jimbo hili, lakini Bashe hajaweza kwa sababu ni msaidizi wangu katika safari hii ya matumaini,” alisema Lowassa.
Naye mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Arusha, Matthias Manga, alimsifu Bashe akisema licha ya kuishi Dar es Salaam, amekuwa karibu na wananchi wa Nzega.
Akitangaza idadi ya wana CCM waliomdhamini Lowassa katika Wilaya ya Nzega, katibu wa Wilaya, Epimark Makwea, alisema wamejitokeza wanachama 3,816.
Akiwa mjini Tabora, Lowassa, aliyepata mapokezi makubwa, alisema anayajua matatizo ya mkoa huo, ukiwemo umasikini uliokithiri.
“Nayajua matatizo ya Tabora; kuna matatizo ya umasikini, reli ya kati na tatizo la maji. Rais Mwinyi (Ali Hassan) alifanya yake, Rais Mkapa (Benjamin) alifanya yake na Rais Kikwete (Jakaya) alifanya yake. Sisemi kwamba walikosea, bali kila mtu alijaribu bahati yake. Ikimpendeza Mungu nikifanikiwa nitaendesha mchakamchaka wa maendeleo,” alisema Lowassa.

Jumla ya wana CCM wa Tabora Mjini waliomdhamini Lowassa walifikia 9,516 ambapo kati yao, 45 ndio wamechukuliwa katika fomu ya udhamini.
Mkutano huo ulisheheni wazee wa CCM, akiwemo Mzee Nkumba, ambaye ni baba yake Mbunge wa Sikonge, Said Nkumba na Mbunge wa Urambo Mashariki, Profesa Juma Kapuya na waziri wa zamani, Tatu Ntimizi.

- Advertisement -
Previous article
Next article

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles