25.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

KLITSCHKO ATANGAZA KUSTAAFU NGUMI

KIEV, UKRAINE

BINGWA wa ngumi nchini Ukraine, Wladimir Klitschko, ametangaza kustaafu ngumi saa chache baada ya Anthony Joshua kudai kuwa anataka kurudiana na mkongwe huyo Novemba, mwaka huu.

Wawili hao walipambana Aprili 29, mwaka huu na Joshua kufanikiwa kuibuka bingwa wa uzito wa juu kwa ushindi wa KO katika raundi ya 11, hivyo siku moja baada ya pambano hilo, Klitschko aliweka wazi kuwa yupo tayari kurudiana na Joshua.

Wiki iliyopita wakala wa Joshua alipeleka maombi kwa uongozi wa Klitschko juu ya kurudiwa kwa pambano, hivyo walikuwa wanasubiri majibu wiki hii, lakini Klitschko tayari ametangaza kustaafu.

Jana Joshua alitumia akaunti yake ya Instagram kudai kwamba anasubiri majibu kutoka kwa uongozi wa Klitschko ili aanze mazoezi ya nguvu Agosti 22, mwaka huu kuelekea pambano hilo lililopangwa kufanyika Novemba, mjini Las Vegas.

“Ninasubiri majibu kutoka kwa uongozi wa Klitschko kuelekea pambano letu ili nianze mazoezi ya nguvu Agosti 22, ninaamini nikifanya kwa miezi mitatu nitakuwa sawa kushinda pambano hilo.

“Sina wasiwasi na bingwa huyo kwa kuwa ninaujua uwezo wake na nilifanya makubwa Aprili mwaka huu dhidi yake, hivyo bado nina nafasi zaidi,” alisema Joshua.

Baada ya kauli hiyo ya Joshua, Klitschko, mwenye umri wa miaka 41, aliamua kujirekodi video na kuisambaza kwenye mitandao ya kijamii, akidai kutangaza kustaa mchezo huo.

“Naomba niweke wazi kwa mashabiki wangu kwamba huu ni wakati wangu wa kustaafu ngumi, nimekuwa kwenye mchezo huo kwa miaka 21, nadhani huu ni wakati sahihi wa kuwapisha wengine waendelee.

“Sina mpango wowote wa kurudi ulingoni, hivyo mashabiki wangu wakae wakijua hilo, bado nitaendelea kuwa shabiki wa mchezo huo kwa kuwa umekuwa sehemu ya maisha yangu,” alisema Klitschko

Kutokana na hali hiyo, uongozi wa Joshua umesema upo kwenye mipango ya kutafuta pambano lingine mwaka huu na kuna uwezekano mteja wao akapambana na bingwa wa mkanda wa IBF, Kubrat Pulev.

“Tumepata taarifa kwamba Klitschko ameamua kustaafu ngumi, Joshua alikuwa na mipango ya kurudiana na bondia huyo, lakini kutokana na hali hiyo tupo kwenye mipango ya kutafuta pambano lingine, kuna uwezekano akacheza na bingwa wa IBF, Kubrat Pulev,” ulisema uongozi wa Joshua

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles