29.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Kerr aibuka Tanga, aisoma African Sports kimya kimya

dylanker-haiphongOSCAR ASSENGA, TANGA NA MWALI IBRAHIM, DAR ES SALAAM
KOCHA Mkuu wa Simba, Dylan Kerr, juzi ametumia muda wa dakika 90 kukisoma kikosi cha timu ya African Sports “Wanakimanumanu”, wakati ikicheza mchezo wa kirafiki na Coastal Union kwenye Uwanja wa Mkwakwani.

Kocha huyo alitua Tanga kimya kimya ili kuweza kukijua vizuri kikosi cha ‘Wana kimanumanu’, kabla hawajakutana kwenye ufunguzi wa Ligi Kuu soka Tanzania bara Septemba 12, mwaka huu.

Mchezo huo wa kirafiki ulimalizika kwa Coastal Union kuibuka na ushindi wa bao 1-0, bao ambalo lilifungwa na Tumba Sued dakika ya 38 baada ya kumalizia kazi nzuri iliyofanywa na Yusuph Sabbo.

Kerr ambaye alikuwa amevalia kofia iliyomfanya asijulikane kirahisi na mashabiki wa soka, aliambatana na Kocha Msaidizi wa timu hiyo, Suleiman Matola, waliingia uwanjani hapo kama watazamaji wa kawaida na kujichanganya na mashabiki wengine wa soka waliokua wakishuhudia mchezo huo.

Mechi hiyo ilikuwa na upinzani mkubwa kutokana na timu zote mbili kukamiana vilivyo kwa lengo la kila mmoja kutaka kuibuka na ushindi ili kuweza kuendeleza rekodi ya ubabe kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.

Kutokana na ushindi walioupata Coastal Union dhidi ya wapinzani wao African Sports, iliwalazimu mashabiki wa timu hiyo kuzunguka kwenye mitaa mbalimbali ya Jiji la Tanga wakishangilia kitendo ambacho kilipelekea kusimamisha baadhi ya shughuli zilizokuwa zikiendelea.

Kivutio katika mchezo huo kilikuwa ni vikundi vya ngoma kutoka kwenye kila timu, ambao waliimba na kucheza huku wakiwa na sare zao maalumu.

Katika hatua nyingine, Kocha Kerr amewataka mashabiki wake wakae mkao wa kula kusubiri kuona kikosi kipya cha Simba kujua nini wanakifanya kwenye kambi yao Zanzibar.

Alisema hataki kukizungumzia zaidi kikosi chake hicho na anawaachia kazi mashabiki kukiona wenyewe na ana imani watakubali.

“Kambi inaenda vizuri kwa ujumla, wachezaji wapo safi, Jonas Mkude, Mohamed Fakhi na Emery Nimuboma wanaendelea vizuri na watajiunga na timu wakati wowote, mashabiki wasubiri waone tu kikosi chao,” alisema.

Simba bado ipo kambini Zanzibar ikijiandaa na ligi kuu, ikiwa katika maandalizi hayo imefanikiwa kucheza michezo 11 ya kirafiki ambapo iliweza kushinda michezo saba mfululizo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles