23.2 C
Dar es Salaam
Saturday, July 27, 2024

Contact us: [email protected]

Kero ya maji Chalinze kuwa historia

Na Mwandishi Wetu, Pwani

Kero ya maji katika vitongoji na vijiji vya Kata ya Kibindu jimboni Chalinze inakusudiwa kuwa historia kutokana na utekelezaji wa miradi ya maji yenye thamani ya zaidi ya Sh bilioni 1.6.

Akizungumza na wakazi wa Kijiji cha Kwamduma jana, Mbunge wa Chalinze (CCM), Ridhiwani Kikwete, amewahakikishia wananchi wa Kata ya Kibindu kuwa kero ya maji inaenda kuwa historia kwa kuwa tayari shughuli za utekelezaji wa mradi huo zinaendelea.

Mbunge wa Chalinze (CCM), Ridhiwani Kikwete (katikati), akifafanua jambo kwa Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Zainab Kawawa (kushoto), wakati wa kukagua miradi ya maji katika Kata ya Kibindu jimboni Chalinze jana. Na Mpigapicha Wetu.

Pia amemshukuru Rais Dk. John Magufuli kwa hatua zinazochukuliwa za kupata ufumbuzi wa kero ya maji katika kata hiyo na Jimbo zima la Chalinze.

“Serikali imejidhatiti kuhakikisha maji yanawafikia wananchi wa Kibindu. Niwahakikishie kuwa miradi hii itakamilika kwa wakati na mapema ili wananchi wapate maji safi na salama,” amesema Ridhiwani.

Pia amesema amefanya jitihada mbalimbali ikiwamo kuchimbwa kwa visima zaidi ya vinne katika vijiji mbalimbali vya kata hiyo ikiwamo Kwamduma vimechimbwa viwili, Kibindi vimechimbwa viwili na Kwamsanja kimechimbwa kimoja na vyote hivyo vimesaidia japo kero ya maji bado haijaisha.

“Uchimbaji wa mabwawa haya makubwa na usambazaji kwenda kwa wananchi unakuja wakati mwafaka, hivyo matarajio ni kwenda kutatua kero ya maji kwa ukubwa huo uliokusudiwa.

“Kwa hakika tuna kiongozi wetu Rais Magufuli ambaye sio tu kwamba anasema mdomoni kuwajali wananchi wanyonge isipokuwa anatenda kwa vitendo,” amesema Ridhiwani.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Zainab Kawawa, amesema Serikali imejidhatiti kuhakikisha maji yanawafikia wananchi wa Kibindu na alimuhakikishia Ridhiwani kuwa mradi huo utakamilika mapema ili wananchi wapate maji safi na salama.

Akielezea utekelezwaji wa mradi huo, Zainab, amesema Serikali imetoa Sh bilioni 1.6 kwa ajili ya miradi yote ikiwamo Sh milioni 700 kwa ajili ya Kijiji cha Kwamsanja na Sh milioni 900 kwa ajili ya Kijiji cha Mjembe.

Pia amesema miradi hiyo inatarajiwa kwa pamoja kutoa lita zisizopungua milioni tatu na nusu zinazokwenda kutatua kero ya maji katika Kata ya Kibindu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles