28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

KAMATI ZA BUNGE KUJADILI MISWADA

KAMATI ZA BUNGE

Na MWANDISHI WETU- DAR ES SALAAM

VIKAO vya Kamati za Kudumu za Bunge vinatarajiwa kuanza Jumatatu ya wiki ijayo mjini Dodoma, pamoja na mambo mengine watajadili miswada ya sheria ya marekebisho mbalimbali.

Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari Dar es Salaam jana na Ofisi ya Bunge Mjini Dodoma, inaeleza kamati hizo zitaanza kukutana Januari 16 hadi 29, mwaka huu kutekeleza majukumu yake kabla ya kuanza kwa mkutano wa sita wa Bunge utakaoanza Januari 31, mwaka huu.

Taarifa hiyo inaeleza kuwa kutokana na ratiba ya shughuli za kamati, wabunge wote wanapaswa kuwasili mjini Dodoma ifikapo kesho tayari kwa kuanza vikao hivyo.

“Katika utekelezaji wake wa majukumu, kamati 12 zitafanya ziara za kukagua miradi ya maendeleo katika maeneo mbalimbali nchini inayotekelezwa na wizara/idara zinazosimamiwa na kamati husika,” ilisema taarifa hiyo.

Pia ilisema ziara hizo zitafanyika kuanzia Januari 17 hadi 21, mwaka huu kabla ya kuendelea na vikao Januari 23, mwaka huu.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, kamati mbili za kisekta zitajadili na kupokea maoni ya miswada mitatu kati ya hiyo miwili itajadiliwa na Kamati ya Katiba na Sheria.

“Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya sheria mbalimbali, namba nne wa mwaka, 2016 (The Written Laws (Miscellaneous Amendments) Bill, 2016) na Muswada wa Sheria ya Huduma ya Msaada wa Kisheria wa Mwaka 2016 (The Legal Aid Bill, 2016).

“Kamati hiyo itakuwa na vikao vya kupokea maoni ya wadau kuhusu miswada hiyo siku ya Januari 19 na 20, mwaka huu

mjini Dodoma kuanzia saa tatu kamili asubuhi hadi saa tisa alasiri,” ilisema.

Taarifa hiyo iliongeza kuwa kamati nyingine itakayochambua muswada ni Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii itakayochambua Muswada wa Sheria ya Madaktari, Madaktari wa Meno na Wataalamu wa Afya shirikishi wa Mwaka 2016 (The Medical, Dental and Allied Health Professionals Bill, 2016).

Taarifa hiyo ilisisitiza kuwa baada ya kuchambua muswada huo kamati itakuwa na vikao vya kupokea maoni ya wadau kuhusu muswada huo Januari 18, mwaka huu mjini Dodoma kuanzia saa tatu kamili asubuhi hadi saa tisa alasiri.

Pia taarifa hiyo iliwataka wadau wote katika miswada kufika mbele ya kamati kutoa maoni yao katika tarehe na muda uliotajwa.

Iliendelea kusema kuwa kuanzia Januari  23 hadi 27, mwaka huu kamati za kisekta zitaendelea kupokea taarifa za kiutendaji za wizara zinazosimamiwa na kamati hizo kwa mujibu wa kifungu cha 7 (1) (c) na (d) cha nyongeza ya nane ya Kanuni za Kudumu za Bunge toleo la Januari, mwaka jana.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles