25.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

JPM ATENGUA UTEUZI WA DED BUTIAMA

Na Mwandishi Wetu – DAR ES SALAAM


RAIS Dk. John Magufuli, ametengua uteuzi wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Butiama, Solomon Ngiliule.

Akitangaza uamuzi huo ofisini kwake Dar es Salaam jana, Waziri  wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Selemani Jafo, alisema amefikia uamuzi huo kutokana na kujiridhisha na makosa yanayodaiwa kutendwa na mkurugenzi huyo.

Mbali ya kutengua uteuzi huo, pia Waziri Jafo amemwelekeza Katibu Mkuu Ofisi ya Rais – Tamisemi, kuchukua hatua sitahiki kwa Mweka Hazina Masanja Sabuni aliyehusika wakati wa matumizi mabaya ya fedha za Serikali.

“Rais Magufuli ametengua uteuzi wa mkurugenzi wa Butiama kutokana na makosa yaliyopo mbele yake, pia ameagiza mweka hazina aliyehusika na upotevu wa fedha za Serikali achukuliwe hatua.

“Nawaomba  watendaji wa wizara hii kufanya kazi kwa weledi na kuzingatia kanuni za utumishi wa umma,” alisema Waziri Jafo.

Uamuzi wa Rais Magufuli, umekuja siku mbili tu, baada ya Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kushtushwa na upotevu wa mamilioni ya fedha katika halmashauri hiyo ambayo imeanzishwa hivi karibuni.

Majaliwa alitoa maagizo wakati wa kikao cha majumuisho ya ziara yake ya siku tano mkoani Mara, akimwagiza Naibu Waziri Ofisi ya Rais (Tamisemi), Josephat Kandege, kubaki Butiama ili kuhakikisha ukaguzi maalumu unafanyika juu ya fedha zinazotumwa na Serikali kwa miradi mbalimbali ya halmashauri hiyo.

Pia alimwagiza Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara, Raphael Nyanda, kutuma timu ya wakaguzi kufanya ukaguzi maalumu katika ofisi ya Solomon Ngiliule, Mweka Hazina wa Halmashauri, Sabuni na Ofisa Manunuzi wa Halmashauri  hiyo, Robert Makendo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles