24.1 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Jamii yatakiwa kuwa na mtazamo chanya kwa wenye ulemavu

Na Vincent Mpepo, OUT

Imeelezwa kuwa watu wanaoishi na ulemavu wana fursa ya kujiingizia kipato na kukuza uchumi binfasi na wa taifa kupitia vipaji vyao ambavyo vinaweza kutumika katika nyanja mbalimbali hususani sekta ya sanaa.

Hayo yameelezwa na Mkurugenzi Mtendaji na Mwanzilishi wa Asasi ya Dhahabu, Dk. Hadija Jilala katika siku ya Tuzo za Dhahabu na Uzinduzi wa Mashindano ya Tuzo za Vipaji vya uvumbuzi na ubunifu kwa watu wenye ulemavu mwaka 2020 zilizofanyika jana katika ukumbi wa Maafisa wa Jeshi la Polisi Msasani jijini Dar es Salaam.

Alisema asasi yake imeamua kufanya kitu hicho ili kuleta hamasa kwa jamii na zaidi kujenga uelewa wa fursa na changamoto wanazozipitia watu wanaoishi na ulemavu wa aina mbalimbali kwa kuweka mkazo kwenye kundi la watoto na vijana ili kuwa na jamii inayotambua masuala ya ulemavu tangu ngazi ya chini.

“Ni tuzo endelevu kwa kuwa zitafanyika kila mwaka ili kuwa kitu kinachoishi na kutambulika kitaifa na kimataifa”, alisema DK. Jilala.

Alisema kutakuwa na mashindano katika shule za msingi na sekondari kwa mashindano ya wazi katika majukwaa na uandishi wa kzai mbalimbali ili kupata na kuibua vipaji mbalimbali tangu ngazi za chini ili kujenga jamii jumuishi kwa siku za usoni.

Katibu Mtendaji wa Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), Godfrey Mngereza alisema jamii inapaswa kuwa na mtizamo chanya kuhusu watu wanaoishi na ulemavu kwa kuwa kila binadamu ana ulemavu na anaweza kuupata muda wowote hivyo kuwa na mtizamo hasi ni tatizo linalosababisha unyanyapaa.

“Hakuna mtu aliyempangia Mungu azaliwe kwa namna yeyote bali ni kitu kinachotokea kwa mapenzi yake”, alisema Mngereza.

Aidha, aliwataka wazazi wenye Watoto wanaoishi na ulemavu kutokuona kuwa wamepewa adhabu au laana kwa kuwa yote ni mapenzi ya Mungu.

Alisema BASATA kama taasisi inayohusika na masuala ya sanaa inaunga mkono tuzo hizo na ipo tayari kushirikiana na Asasi ya Dhahabu ili kuhakikisha masuala ya watu wanaioshi na ulemavu yanapatiwa ufumbuzi kama sehemu ya ushiriki wa moja kwa moja wa serikali kwa jamii jumuishi.

Msanii wa Muziki wa kizazi kipya, Elias Barnabas (Barnaba) alisema sanaa ni kitu kinacholipa ikiwa wahusika watakichukulia kwa uzito wake hivyo kutimiza ndoto ndoto zao kupitia sanaa kama ujira.

“Tusiichukulie sanaa kama ujira wa masihara, bali tuione kama ni fursa ambayo itatufikisha kwenye kuziishi ndoto zetu,” alisema Barnabas.

Aliwaasa watoto na vijana wanaoishi na ulemavu ambao wana vipaji katika uga wa sanaa mbalimbali kutokata tamaa na kuwa makini kwa wakifanyacho bila kuyumbishwa na upepo wa aina nyingine ya sanaa ili kukulia kwenye lengo na mahitaji ya sanaa waipendayo

Wakati wa uzinduzi wa tuzo za Dhahabu washiriki walijionea vipaji mbalimbali kutoka kwa wanaoishi na ulemavu ikiwemo uimbaji wa nyimbo za injili na Bongo Fleva, uigizaji, utunzi na kughani mashairi na utangazaji.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles