21.5 C
Dar es Salaam
Saturday, July 27, 2024

Contact us: [email protected]

JAJI MKUU: MAHAKAMA INATEKELEZA MAJUKUMU YAKE KWA VITENDO

NA KULWA MZEE – DAR ES SALAAM


JAJI Mkuu Profesa Ibrahimu Juma, amesema mahakama inatekeleza majukumu yake kwa vitendo, kuwajengea uwezo watumishi wake na wadau wengine wa sheria.

Alisema hayo jana Dar es Salaam wakati akizindua kituo cha kihistoria cha mafunzo na habari za mahakama Kisutu, kitakachotoa mafunzo kwa njia ya mtandao kwa vituo vitano nchini kwa wakati mmoja.

“Mahakama inatekeleza majukumu yake kwa vitendo, kuwajengea uwezo watumishi wa mahakama na wadau wengine wa sheria kwa sababu kuna mambo mengine hawakusoma wakiwa chuoni.

“Tehama inarahisisha kazi kwa sababu kutoa haki kwa kutumia Tehama, tunawafikia wananchi wengi kwa urahisi zaidi,” alisema.

Akizindua kituo hicho jana, Jaji Juma alisema kimejengwa kwa kushirikiana na Benki ya Dunia.

Alisema kituo kina malengo ya kuhakikisha haki inawafikia wananchi na walengwa kwa urahisi zaidi na kwa wakati.

Jaji Juma alisema kuna maeneo mapya yanayohitaji mafunzo kwa watumishi wa mahakama ikiwemo makosa ya mtandao, yanayotokana na miamala ya simu na dawa za kulevya.

Alisema mahakimu na waendesha mashtaka wakipata mafunzo hayo watakuwa na uelewa mmoja katika kutoa haki.

Jaji Juma alisema makosa hayo yanahitaji ushiriki wa vyombo vya nje, kuna sheria nyingi za kimataifa zinagusa sheria za Tanzania.

Akizungumzia utendaji kazi wa kituo hicho, Mkuu wa Chuo cha Mafunzo ya Sheria Lushoto, Jaji Dk. Paul Kihwelo, alisema kinaweza kuendesha mafunzo kwa vituo vitano kwa pamoja.

“Mafunzo yanaweza kutolewa hapa, lakini Lushoto, Mbeya na Bukoba wakashiriki kupitia mtandao kwa sababu wamefunga mtambo unaowezesha mafunzo kuendelea kwa mtandao.

“Hata kwa sekta binafsi kama wanahitaji kutumia kituo lakini wanahitaji kushirikiana na wenzao nje ya kituo, inawezekana kama huko waliko kumefungwa mtambo huo,” alisema Jaji Kihwelo.

Alisema kwa mara ya kwanza mahakama imejenga kituo cha mafunzo na kwamba kuanzishwa kwa kitengo hicho ni msingi mzuri wa kuwapo kwa uhuru wa mahakama kwa kuwajengea uwezo watumishi.

Jaji Kihwelo alisema mafunzo ya mwanzo ya tehama yatatolewa kwa wadau mbalimbali wakiwamo wanafunzi, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) na TRA,” alisema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia, Bella Bird, alisema mfumo huo utasaidia kuwafikia wananchi wengi kwa urahisi zaidi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles