25 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Jaji Lubuva: Nilipata vitisho wakati wa Uchaguzi Mkuu 2015

Jaji Lubuva
Jaji Lubuva

NA ESTHER MNYIKA

UCHAGUZI Mkuu wa mwaka jana ulikuwa na ushindani mkubwa, ambapo hadi dakika za mwisho ilikuwa vigumu kujua mshindani ni nani.

Ushindani huo ulitokana na vyama vinne vya upinzani kuungana na kuanzisha umoja wao huku mawaziri wakuu wa zamani, Edward Lowassa na Frederick Sumaye wakijiunga na vyama hivyo.

Hamasa ilizidi pale Lowassa alipotangazwa kuwa mgombea urais wa vyama hivyo vya upinzani, lakini baadaye mgombea wa CCM akatangazwa kuwa mshindi.

Gazeti hili limefanya mahojiano na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi (NEC), Jaji Joseph Lubuva ambapo pamoja na mambo mengine anasema alipata vitisho wakati wa kutangaza matokeo.

MTANZANIA: Umekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi (NEC) kwa muda mrefu, je unakumbana na changamoto zipi?

JAJI LUBUVA: Katika ofisi zote nilizopata kuzisimamia na kufanya kazi, NEC imekuwa na changamoto nyingi kwa sababu ni sehemu ambayo inagusa maisha ya watu moja kwa moja.

Pamoja na changamoto hizo, zingine tumejitahidi kuzitatua kwa kushirikiana na makamishna wenzangu.

Wakati mgumu zaidi ni pale wagombea, kila mmoja anatoa majibu yake kuwa eti fulani amependelewa, kunakuwa na maneno mengi lakini mwisho wa siku lazima mshindi apatikane kutokana na kura za wananchi kwa sababu ndio waliomchagua kwa kuona anafaa kuwatumikia.

Nimejifunza mengi kuhusu uchaguzi; tumekuwa na ushirikiano na tume nyingine. Tume ya Tanzania ni tume inayoaminika kuna msemo unasema ‘nabii hasifiwi nyumbani’ ila tukitoka nje tunasifiwa.

Mapungufu yapo kila mahali yanatakiwa kuboreshwa mbele ya safari, uchaguzi umekwisha na tayari tumetoa ripoti ya uchaguzi wa mwaka 2015 ndio hatua ya mwisho…sasa tunaanza kuangalia mambo ya msingi.

MTANZANIA: Katika uchaguzi uliopita watu wa makundi maalumu hasa wenye tatizo la usikivu waliilalamikia Tume kutowawekea wakalimani katika mikutano ya kampeni  hadi Uchaguzi Mkuu, hili unalizungumziaje?

JAJI LUBUVA: Nakubali malalamiko hayo yapo lakini ni mapungufu ya kawaida kama makundi maalumu wakati wa kupiga kura vifaa vyote vilikuwepo hakuna ambaye hakupiga kura, vyama vya siasa vilipaswa kuweka wakalimani kwenye mkutano yao wakati wa kampeni.

MTANZANIA:  Kwanini mlirudisha fedha zilizobaki kwenye Uchaguzi Mkuu, wakati kulikuwa na upungufu wa vifaa?

JAJI LUBUVA: Fedha ambayo imerudishwa ilianza kuombwa serikalini kwa ajili ya maandalizi ya uchaguzi kuanzia mwaka 2012, 2013 na 2014.

Mwaka 2013 na 2014 katika bajeti hatukupata fedha kwa ajili ya maandalizi ya uchaguzi, hivyo uchaguzi unakaribia ndio tunapata fedha hiyo.

Fedha za uchaguzi zinakuja kwa kuchelewa kutokana na hilo, mambo mengine hatukufanya kama ilivyopangwa kwenye mikakati yetu mfano; tulipanga kufanya mikutano 20 kutokana na fedha kuchelewa tukafanya 15 na fedha ikabaki.

Sisi ni waaminifu ile fedha itatumiwa kujenga ofisi yetu ambayo tumepewa na Rais John Magufuli na tutaijenga Dodoma, ambayo itakuwa na eneo kubwa tofauti na hapa tulipo sasa.

MTANZANIA:  Wakati wa kutangaza matokeo ya Uchaguzi Mkuu hukupata vitisho?

JAJI LUBUVA: Hapana kwa ujumla tulifanya kazi ile kwa uwazi zaidi kwa kuhakikisha matokeo yanabandikwa katika kila kituo lakini vitisho vilitokea kwenye mitandao ya kijamii, watu walikuwa wanatishia maisha yangu hivyo walifikishwa mahakamani.

MTANZANI: Wakati ule kulikuwa na malalamiko kuwa matokeo uliyotangaza si yale yaliyokuwa vituoni, unayazungumziaje malalamiko haya?

JAJI LUBUVA: Kila kituo kulikuwa na mawakala waliokuwa wanasimamia na hatukupata malalamiko kutoka kwa mawakala na matokeo waliyotuma ndio tuliyotangaza, hakuna mgombea yeyote tuliyemkandamiza na hatukupendelea mtu yeyote.

MTANZANIA: Unazungumziaje malalamiko kwamba NEC haiku huru kutekeleza majukumu yake?

JAJI LUBUVA: Tume ipo huru, ni lazima waelewe kwamba haipaswi kuingiliana na mtu yeyote katika utendaji kazi wake, hakuna hata siku moja Rais ameiingilia tume, ipo huru na inafanya kazi kwa mujibu wa sheria.

Katiba inayopendekezwa kuna mambo ya tume huru yapo ila wajumbe wasiteuliwe wa vyama vya siasa wateuliwe kwa sifa mfano Kenya walikuwa wakilalamika kuwa tume haipo huru wakaunda tume nyingine ambayo ilikuwa na wanasiasa matokeo ndio hayo yanayotokea wanataka tena tume ya zamani irudishwe.

MTANZANIA: Kumekuwa na malalamiko kwa wagombea kuwa mnagawa majimbo makubwa ambayo yanagharimu fedha nyingi wakati wa kampeni hadi inapitiliza bajeti iliyopangwa  na Msajili wa Vyama vya Siasa.

JAJI LUBUVA: Kila uchaguzi unaokuja tunafanya zoezi la kugawanya majimbo na hadi tunagawanya, jimbo linakuwa limekidhi vigezo vinavyotakiwa mfano tunaangalia ongezeko la watu.

MTANZANIA: Nini maoni yako, je unaunga mkono Katiba inayopendekezwa ya Bunge Maalumu la Katiba au ile ya Jaji Joseph Warioba?

JAJI LUBUVA: Aprili mwaka jana alileta Katiba pendekezi sheria namba 11 ya mwaka  1973, inafanya kura ya maoni kuna mambo yabainishwe kwenye kura ya maoni.

ZEC na NEC ni muungano kwa pamoja tukae tuangalie vifungu vipi vimefuatwa na baada ya hapo kazi inaanza, kwa sasa tunasubiria ZEC itoe ripoti ya uchaguzi tuendelee na zoezi hilo.

Kuangalia kwa pamoja katiba inayopendekezwa tunapeleka serikalini Bunge lifanye marekebisho katiba pendekezi ni matokeo ya tume ya Warioba ambayo imepelekea kuwepo kwa Bunge Maalumu.

MTANZANIA : Nini ushauri wako  kwa Serikali katika chaguzi zijazo?

JAJI LUBUVA: Naishauri Serikali kuwa na mfuko wa uchaguzi kila mwaka wa fedha  kuwe na kiwango fulani.

Hiyo itasaidia kutocheleweshewa fedha za uchaguzi na kufanya kila kitu kwa wakati kutokana na kuwa fedha ipo ikiwa tofauti na chaguzi zilizopita.

MTANZANIA: Wewe kitaaluma ni mwanasheria, unazungumziaje hoja ya Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Rushwa (Takukuru) ya kutaka kupewa uwezo wa kumfikisha moja kwa moja mahakamani mtuhumiwa wa rushwa pale wanapomkamata?

JAJI LUBUVA: Siungi mkono hoja hiyo kwamba kesi ziwe zinakwenda moja kwa moja mahakamani, kuna mambo mengi yanapendekezwa lakini ni vigumu…kuiondoa Ofisi ya DPP kusimamia hilo ni muhimu kwa wao kupitia mafaili hayo kabla ya kupelekwa mahakamani.

Kila kitu kina wakati wake, kuna baadhi ya vitu vinafanyiwa mabadiliko kwa mfano; suala la mahakama ya mafisadi kuanzishwa, ni hatua muhimu inaanzishwa sasa lakini sheria zilikuwepo wakati wote.

Ni suala la nchi zote zenye kuamini sheria ofisi ya DPP  ni muhimu na inastahili kuwapo na ni lazima Takukuru ipeleke mafaili kwa DPP yapitiwe ndipo yapelekwe mahakamani.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles