ESTHER MNYIKA NA ASIFIWE GEORGE, DAR ES SALAAM
JAJI mstaafu Mark Bomani, amesema ili kumaliza dosari zilizojitokeza wakati wa uchaguzi mkuu kisiwani Zanzibar, njia pekee ni kuunda jopo litakaloweza kumaliza mgogoro uliopo.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Jaji Bomani alisema dosari zinazosemekana zilitokea wakati wa uchaguzi zinatakiwa zibainike kwa kutumia jopo la wataalamu ambao wanaaminika na ikiwezekana liwe chini ya mmoja wa majaji wakuu wastaafu.
Alisema yaliyotokea Zanzibar ni utata mtupu, hasa baada ya Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Jecha Salim Jecha, kufuta matokeo ya uchaguzi katika mazingira ya kutatanisha.
Jaji Bomani alisema si vibaya kama ZEC itashirikina na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ili kupata wataalamu wa mambo ya uchaguzi kutoka taasisi za kimataifa.
“Jopo hili likibaini na kuzifanyia kazi dosari zilizojitokeza, daftari la kudumu la wapigakura lipitiwe kwa umakini ili uchaguzi urudiwe mara moja,” alisema.
Aidha alimwomba mgombea urais wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad asijitangaze mshindi wala asiogope uchaguzi kurudiwa.
Kuhusu mchakato wa Katiba mpya, Jaji Bomani alisema jitihada zilizoanzishwa mwaka 2012 na Rais mstaafu Jakaya Kikwete zinapaswa kuendelezwa baada ya kugonga mwamba.
Alisema mchakato huo, ulitumia mamilioni ya fedha, kamwe hauwezi kuachwa hivi hivi kwa sababu utakuwa ni uharibifu wa fedha za walipakodi wa nchi hii.
“Nina imani jambo hili litafanikiwa kwani uzoefu wa masuala hayo tunao wa kutosha kuhitimisha mchakato huo,” alisema.