25.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Chadema: Hatutambui zuio la IGP

mangu2NA AGATHA CHARLES, DAR ES SALAAM

SIKU moja baada ya kuahirishwa ziara ya aliyekuwa mgombea urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa, chama hicho kimesema hakilitambui zuio la kufanya maandamano na mikutano ya kisiasa lililowahi kutolewa na Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali (IGP) Ernest Mangu mwezi uliopita.

Kauli ya Chadema ilitolewa jana na Ofisa Habari wa chama hicho, Tumaini Makene, baada ya kuulizwa na MTANZANIA juu ya kuwapo taarifa kuwa wameshindwa kuendelea na ziara ya Lowassa kutokana na zuio hilo.

Akizungumza Dar es Salaam jana, baada ya kuahirishwa mkutano na waandishi wa habari, Makene alisema katazo hilo la mikutano ya hadhara linaendelea.

“Hatulitambui tamko la IGP, sisi tuliahirisha kutokana na kutingwa na shughuli za uchaguzi mdogo, hivyo tukimaliza kushughulikia masuala hayo ya uchaguzi, tutarudi kuendelea na ziara kama tulivyopanga nchi nzima. Hata kama IGP kakataza, mbona CCM wanafanya mikutano ya hadhara?” alisema Makene.

Akizungumzia sababu za kuahirisha mkutano ambao chama hicho kiliuitisha jana na kusababisha waandishi wa habari kusubiri kwa zaidi ya saa tatu, Makene alisema kuna masuala ya msingi ambayo yalijitokeza katika suala la umeya wa Jiji la Dar Salaam ambalo ndilo lilikuwa ajenda.

“Tumeahirisha kwa sababu kuna figisufigisu tumefanyiwa kwenye umeya, hivyo tunazifanyia kazi,” alisema Makene.

Alisema lengo la kuita waandishi wa habari ilikuwa ni kutangaza jina la mgombea wa nafasi hiyo ya umeya wa Jiji la Dar es Salaam.

Mkutano wa viongozi hao ulikuwa ukiendelea ndani ya ofisi za chama hicho, huku kila mara baadhi ya viongozi wakitoka na kutoa matumaini kwa waandishi kuwa mkutano wao utaanza punde.

MTANZANIA liliwashuhudia baadhi ya viongozi wakiingia ndani ya ofisi hizo akiwamo Naibu Katibu Mkuu Zanzibar, Salum Mwalimu, Naibu Katibu Mkuu Bara, John Mnyika, Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake (Bawacha) ambaye pia ni Mbunge wa Kawe, Halima Mdee na wengine.

Mwezi uliopita, Jeshi la Polisi kupitia msemaji wake Advera Bulimba, lilipiga marufuku maandamano na mikutano kutokana na kudai kuwa tathimini iliyofanyika ilionyesha bado kuna mihemuko ya kisiasa ambayo itasababisha uvunjifu wa amani.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles