33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Jaji atumia tochi ya simu kurekodi kumbukumbu

wakiliNA JANETH MUSHI, ARUSHA

JAJI Gadi Mjemas wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Arusha, amelazimika kutumia tochi ya simu kuandika taarifa za kesi ya utakatishaji fedha inayomkabili Wakili Median Mwale na wenzake watatu baada ya umeme kukatika mara mbili wakati kesi hiyo ikiendelea.

Hali hiyo ilitokea juzi wakati mawakili wa pande mbili wakibishana kisheria ambapo ghafla umeme ulikatika na kulazimu kutumia tochi za simu zao huku askari polisi akitumia simu yake kummulikia Jaji Mjemas aweze kuandika taarifa hizo.

Kesi hiyo jana ilisikilizwa ambapo shahidi wa kwanza wa upande wa Jamhuri, SP. Fadhili Mdemu (39) alidai mahakamani hapo kwamba washitakiwa hao walifanya jaribio la kuchepusha kiasi cha dola za Marekani milioni 17.2.

Kesi hiyo iliyochukua miaka minne ilianza kusikilizwa juzi kwa mara ya kwanza saa 7 mchana hadi saa 1:40 usiku.

Shahidi huyo ambaye ni Ofisa wa Idara ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai, Kitengo cha Uhalifu wa Fedha (FCU), alidai kuwa watuhumiwa hao walitaka kuingiza fedha hizo kwenye akaunti ijulikanayo kama East Africa Malaria and HIV Support Program iliyopo Benki ya CRDB, Tawi la Meru jijini Arusha.

Akiongozwa na Wakili wa Serikali, Oswald Tibabyakomya, shahidi huyo alidai fedha hizo zilitolewa kama sehemu ya msaada na taasisi ya kimataifa ya Global Fund kwa ajili ya kupambana na ugonjwa wa malaria na Ukimwi.

Shahidi huyo alidai kuwa fedha hizo zilipaswa kupelekwa kwenye akaunti ya Serikali (Tanzania) iliyopo City Bank nchini Marekani chini ya usimamizi wa Wizara ya Fedha.

“Badala yake watuhumiwa walitaka kuzichepusha na kuwaelekeza wafadhili kwamba fedha hizo zinatakiwa kutumwa kwenye akaunti ya mradi ya CRDB,” alidai shahidi huyo na kuongeza:

“Watuhumiwa walighushi barua iliyoonyesha imetoka kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha wakati huo, Ramadhan Khijjah, ikieleza kuwa safari hii Serikali ya Tanzania imeamua fedha hizo za msaada ziende kwenye akaunti ya mradi ya CRDB badala ya kutumwa kwenye akaunti ya Serikali.

Alidai kuwa wakati Global Fund ikiwa kwenye matayarisho ya mwisho ya kutuma fedha hizo, Wizara ya Fedha ilitoa maelekezo kwao ikidai kama kungekuwapo na mabadiliko ya akaunti ya kutuma fedha hizo wangejulishwa utaratibu wa kufanya ikiwamo kujaza fomu maalumu.

“Nilifanikiwa kupata nyaraka husika, picha zao na anuani ya Posta 2122 Arusha ikionyesha wanapatikana eneo la Unga Ltd jijini Arusha. Taarifa hizo hazikutosha kuwapata wenye akaunti hiyo waliojulikana kama Michael Crispine Chacha na Joseph Anderson Marwa ambapo barua ya kuwatambulisha ilitoka ofisi ya JJ Mwale na kusainiwa na Wakili Mwale,” alidai shahidi huyo.

Baada ya ushahidi huo, Jaji Mjemas aliamuru upande wa utetezi unaoongozwa na Wakili Omary Omary na wenzake wapitie nyaraka hizo.

Hata hivyo, mawakili hao waliomba mahakama isipokee nyaraka hizo kama kielelezo kwa madai kuwa nyaraka hiyo hazikuwa kwenye orodha ya vielelezo vilivyotajwa na upande wa mashtaka.

Mawakili hao walidai kuwa shahidi si muhusika wa kutoa nyaraka na hawana ushahidi wa kimaandishi kama nyaraka hizo zilipatikana kwa kufuata sheria.

Mawakili wa Serikali wakiongozwa na Tibabyakomya waliiomba mahakama ipokee vielelezo hivyo kwani vimekidhi vigezo na matakwa ya kisheria.

Baada ya kusikiliza hoja hizo, Jaji Mjemas aliahirisha kesi hiyo hadi atakapotoa uamuzi wa pingamizi hizo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles