24.1 C
Dar es Salaam
Sunday, July 7, 2024

Contact us: [email protected]

Diwani Kata ya Ilala ajivunia utekelezaji wa Ilani

Na Winfrida Mtoi, Mtanzania Digital

Diwani wa Kata ya Ilala Saady Kimji na  viongozi wengine wa Chama cha Mapinduzi(CCM) wa Kata hiyo wametembelea miradi mbalimbali,  huku akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya chama hicho  kwa kipindi cha 2023 hadi 2024.

Akizungumza katika kikao cha Halmashauri Kuu ya Kata ya Ilala leo Julai 4, 2024 wakati wa kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Ilani Kimji ametaja baadhi ya miradi  iliyotekelezwa ikiwamo sekta ya afya kwa  kujenga zahanati ya Bungoni iliyogharimu Sh. milioni 358 ambapo  Serikali imeshirikiana na taasisi ya Afrika  Relief Organization na  Ubalozi wa Kuwait.

Ameeleza kuwa zahanati  hiyo imeendelea kuboreshwa hasa katika vifaa tiba ambapo kupitia ziara hiyo ya kutembelea miradi walitoa vifaa mbalimbali ikiwamo Utra Sound. 

“Kata yetu ya Ilala kwa sasa ina zahanati ya kisasa inatoa huduma masaa 24 ikiwemo huduma za mama na mtoto,pia sekta ya elimu  Ilala tumejenga na kukarabati shule,” amesema.

Amezitaja baadhi ya shule hizo kuwa ni   shule za  msingi Amana,  Boma,  Ilala, Mkoani, shule ya Sekondari Msimbazi , shule ya Msimbazi Mseto na kujenga shule ya Msingi Mzizima  ambayo ni English Medium.

Ameeleza kuwa shule ya Sekondari Msimbazi ni miongoni mwa shule za mwanzo za Kata, hivyo wameona ni muhimu kuboresha jengo la shule hiyo na lengo ni kuwepo kwa kidato cha tano na sita.

Naye Mwenyekiti wa CCM  Kata ya Ilala, Habibu Nassa, amesema wanafurahishwa na maendeleo yanayofanywa na Serikali  kutokana na jinsi Rais Dk.Samia Suluhu Hassan anavyopambana.

“Tupeleke pongezi zetu kwa mheshimiwa Rais, kwa kweli anapambana kuhakikisha anailetwa nchi yetu maendeleo, pia mheshimiwa  Mbunge wetu. Maendeleo yanakuja pale sisi wenyewe tunapokuwa tayari kwa kweli tumefarijika na kilichofanyika katika Kata yetu,” amesema.

Naye  Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Msimbazi, Michael   Msomba, amesema kiasi cha  fedha walizopewa kwa ukarabati wa madarasa 16, ni Sh. milioni 38 na wanatarajia kukamilisha Septemba, 2024.

Kwa upande wake Daktari Mfawidhi wa zahanati ya Bungoni, Ester Waziri, ameeleza kuwa kwa sasa wanajivunia kukua kwa zahanati hiyo kwani wamefikia kutibu wagonjwa 1000, hali inayochangiwa na uwepo wa vifaa vya kisasa.

Aidha Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Mzizima,  ametaja changamoto inayowajabiri ni uwepo wa gereji karibu na shule hiyo, hali inayotia hofu kuhusu usalama wa walimu na wanafunzi.

Mradi mwingine waliotembelea ni uwanja wa soka wa watoto wenye umri chini ya miaka 13 kwenye shule ya Msimbazi Mseto uliojengwa kwa ushirikiano wa ubalozi wa Uturuki kutokana na ushawishi wa Nahodha wa timu ya Taifa, Mbwana Samatta kupitia Samatta Foundation.



- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles