22.8 C
Dar es Salaam
Thursday, April 18, 2024

Contact us: [email protected]

CWT yaadhimisha miaka 28, yaikumbusha Serikali stahiki za walimu

Na Ramadhan Hasan, Dodoma

CHAMA cha Walimu Tanzania (CWT) kimeadhimisha miaka 28 tangu kuanzishwa kwake huku kikiiomba Serikali kuangalia mambo kadhaa yanayohusu walimu ikiwemo stahiki zao, upandishwaji wa madaraja na bajeti kwa ajili ya uhamisho wa walimu.

Pia kimeweka  wazi mafanikio ambayo kimeyapata ndani ya miaka 28 kuwa ni pamoja na kujenga majengo ya ofisi katika ngazi za Taifa, Mkoa na Wilaya, kuwa na uhusiano mzuri na wanachama wake, kuanzisha Benki ya mwalimu (MCBL).

Hayo yameelezwa leo jijini Dodoma na Kaimu Rais wa Chama hicho, Dinnah Mathamani wakati akizungumza na Waandishi wa Habari katika maadhimisho hayo.

Kaimu Rais huyo amesema walimu wanamadai mbalimbali yasiyo ya mshahara na yale ya mshahara ikiwemo suala la uhamisho hivyo wanaiomba serikali kuyaangalia kwa umakini madai hayo.

“Kweli tuna mafanikio makubwa, kwa miaka 28 tumepambana tumefanikiwa mpaka hapa tulipo kwa mambo ambayo tumeelezwa pamoja na mafanikio mengi bado tuna changamoto hivyo niieleze serikali waajiri wetu katika halmashauri zetu waliopo katika Halmashauri zetu na taasisi zingine zinazomshughulikia mwalimu.

“Kwanza nikieleza suala la stahiki za mwalimu bado mwalimu anamadai mbalimbali yasiyo ya mshahara na za mshahara nikieleza suala la uhamisho sisi kama chama cha walimu hatukatai wakati mwingine uhamisho unatokea ili kuweza kuleta tija na ufanisi sehemu za kazi.

“Lakini serikali iliishasema unapomwamisha mtumishi hakikisha na maslahi yake tayari umeweka sawa lakini tumeeona waajiri wetu wanasema kurekebisha ikama lakini Je umeishamwandalia haki zake? tumewasiliana na wilaya mbalimbali walimu bado wanadai waliopo hapa ni mashuhuda.

“Sasa tunaiomba serikali lakini kwa ajili hasa katika halmashauri tuhakikishe tunaweka bajeti kwa ajili ya uhamisho zinazostahili si vyema kumwangaisha mwalimu anatoka sehemu moja kumpandisha maroli halafu unategemea akafanye kazi akiwa ametulia.

“Apate fedha zake za uhamisho ndio ahame Serikali wakati mwingine inatoa maelekezo mazuri lakini utekelezaji ndio unaleta shida leo tunawaambia kuna Halmashauri zinafanya vizuri kuna halmashauri zinafanya vibaya siku tutaleta mbele ya viongozi lakini pia ndani ya serikali kwamba watu mliowapeleka kule hawawajibiki ipasavyo,” amesema.

Pia amesema changamoto nyingine ni suala la malipo ya likizo pamoja na upandishwaji wa vyeo kwa walimu.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa CWT, Deus Seif amesema chama hicho ni moja kati ya vyama imara vya wafanyakazi ambapo amedai wanajivunia kutetea na kusimamia vyema maslahi ya wanachama wake.

“Tumechagua kukaa meza moja na Serikali badala ya kuandamana na kwa hakika tumefanikiwa zaidi katika majadiliano kuliko katika maandamano. CWT tuna uhusiano mzuri na Serikali. Tunaishukuru Serikali kwa kutupa nafasi ya kukaa mezani na kujadiliana,”amesema Seif.

Naye, Mwekahazina wa Chama hicho, Abubakari Allawi amesema katika miaka 28 ya uhai wa CWT imejenga na inaendelea kujenga majengo kwa ajili ya matumizi ya ofisi katika ngazi za Taifa,Mkoa na Wilaya.

Mwekahazina huyo amesema mpaka sasa wana majengo 20 yanayotumika katika ofisi za chama  za Mikoa ambapo amedai majengo mengine matano katika Mikoa ya Simiyu,Geita,Njombe,Katavi, na Songwe yapo katika hatua za mwisho za ujenzi.

Anasema CWT inajenga majengo 38 ya ofisi katika ngazi za Wilaya ambayo yamegharimu zaidi ya Sh milioni 315.

Amesema katika kipindi cha miaka mitatu  majengo ya Mikoa 19 ya Wilaya yamefanyiwa ukarabati wa shilingi milioni 250 ambapo amedai tangu Ofisi za CWT zilipohamia Dodoma shughuli za Kitaifa zimekuwa zikifanyika katika jengo la Mkoa.

“Chama kimepanga kuanza ujenzi wa jengo la makao makuu mwaka 2022 na tutaendelea kukamilisha majengo matano ya Mikoa na 38 ya Wilaya ambayo yapo katika hatua za mwisho za ujenzi,”amesema.

Amesema kwa kipindi kinachoanza mwaka 2022 majengo mengine ya Wilaya yataanza kujengwa kwa kutumia mfumo wa Force Akaunti ili kupunguza gharama za ujenzi ukilinganisha na utaratibu wa kutumia mkandarasi,”amesema.

Amesema jengo pekee la CWT linalotumika kama kitega uchumi ni mwalimu House.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles