23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

CHADEMA WAIJIBU NEC BAADA YA TAMKO LA MAREKANI

Mwandishi wetu – dar es salaam


CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema),  kimedai Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), inahalalisha vurugu wakati wa uchaguzi kutokana na taarifa yake iliyotoa kujibu tamko la Ubolazi wa Marekani nchini, iliyoeleza kutoridhishwa na namna uchaguzi mdogo wa Agosti 12 ulivyoendeshwa.

Taarifa ya Chadema iliyotolewa na msemaji wa chama hicho, Tumaini Makene, ilisema uchaguzi si tukio la siku moja, bali ni mchakato, hivyo dunia ilianza kufuatilia mchakato wake kupitia njia mbalimbali.

“Chadema ilijitokeza tangu mwanzo kuelezea namna ambavyo kulikuwa na ukiukwaji wa Sheria ya Uchaguzi na kanuni zake, hali ambayo ilikuwa ni dalili ya kuwepo kwa mipango na hujuma za kuvuruga na kuharibu uchaguzi, hivyo kutokuwa huru na haki.

“Ni aibu kubwa na dalili mbaya kwa mwenendo wa misingi ya utawala bora kwa nchi yetu, kujaribu kuwahadaa Watanzania na jumuiya ya kimataifa kuwa kilichofanyika katika uchaguzi wa marudio wa Agosti 12 na zingine kabla ya hapo kuwa ni uchaguzi huru na haki.

“Ni kweli kuwa Tanzania ni nchi huru, lakini uhuru huo unaenda sambamba na wajibu wa kusimamia, kutekeleza na kuendesha masuala yake kwa kuzingatia mambo muhimu kama kulinda haki za binadamu, katiba ya nchi na sheria zake, sheria za kimataifa na mikataba mbalimbali ambayo Tanzania imesaini na kukubaliana nayo.

“Ni vyema Serikali ya Tanzania kwa ujumla wake na watumishi wa umma waliopewa mamlaka katika vyombo mbalimbali, wakatambua kuwa vitendo vya uvunjifu wa haki za binadamu, sheria na katiba ya nchi vinavyofanyika bila hatua yoyote kuchukuliwa dhidi ya wahusika, vinaangaliwa na kufuatiliwa na jamii ya Watanzania na dunia nzima.

“Ndiyo maana mara kadhaa tumekuwa tukiwatahadharisha watumishi wa umma wanaokubali ‘kutumika’ au wanaojituma wenyewe kufanya na kutekeleza vitendo hivyo kuwa iko siku watawajibika mbele ya sheria, ama katika vyombo vya ndani au vya kimataifa, wao wenyewe kwa matendo yao. Kwa sababu dunia inafuatilia na inajua,” ilisema taarifa hiyo ya Chadema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles