24.4 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

Busu la Papa Francis lamponya uvimbe mtoto

2EB7459800000578-0-image-a-78_1448248918588PHILADELPHIA, Marekani

KIONGOZI wa Kanisa Katoliki Duniani, Papa Francis, anasadikiwa kufanya muujiza baada ya kumbusu mtoto mwenye umri wa mwaka mmoja aliyekuwa akisumbuliwa na maradhi ya uvimbe kwenye ubongo.

Muujiza huo unadaiwa kufanywa na Papa, wakati wa ziara yake katika Jimbo la Philadelphia, nchini Marekani, Septemba mwaka jana.

Vyombo vya habari nchini Marekani tayari vimefanya mahojiano na wazazi wa mtoto huyo anayeitwa Gianna Masciantonio na kukiri baada ya Papa kumbusu mtoto huyo uvimbe huo umepotea.

Uvimbe wa Gianna ilisemekana hauwezi kutibika, hasa baada ya kufanyiwa operesheni nane na hata kupewa matibabu mengi  ya mionzi (chemotherapy),  akiwa na umri wa miezi 15 tu  katika hospitali ya watoto ya Philadelphia.

Tayari madaktari walikwishatoa ripoti yao kwamba hataweza kupona na zaidi wakimpa miezi kadhaa tu ya kuishi.

 

JINSI WALIVYOMFIKIA PAPA

Wazazi wa mtoto huyo, Joey Masciantonio na Kristen waliarifiwa juu ya ujio wa Papa katika jimbo wanaloishi la Philadelphia na rafiki yao ambaye ni wakala wa FBI, Donny Asper.

Wakala huyo wa FBI alikuwa amepewa jukumu la kuimarisha ulinzi akiwa na maofisa wenzake zaidi ya 100 katika ziara hiyo ya Papa.

Inaelezwa wakala huyo wa FBI aliwaelekeza wazazi hao kufika haraka iwezekanavyo karibu na eneo la kihistoria la James S. Byrne, ambako Papa alikuwa akitarajiwa kupita baada ya kuhutubia katika ukumbi wa Uhuru.

Joey na familia yake walifika katika eneo hilo na baba huyo wa mtoto anasema alimnyanyua juu Gianna ili maofisa wa Polisi na mawakala wa FBI waweze kumuona kama alivyoelekezwa na  Asper.

Pamoja na kwamba mama wa mtoto huyo, Kristen, alikuwa akitamani binti yake huyo kukutana na Papa, lakini wakala huyo wa FBI ndiye aliyehakikisha Joey, mkewe pamoja na watoto wao wawili wanafanikiwa kupita mbele kumuona kiongozi huyo wa kiroho ambaye alimbusu Gianna kichwani na kisha kumshika kama ishara ya kumbariki.

 

WANACHOSEMA WAZAZI

Kwa mujibu wa mahojiano yaliyofanyika wiki iliyopita kati ya kituo cha NBC-News na wazazi wa mtoto huyo ambao wote ni waumini wa Kanisa Katoliki, uvimbe uliokuwa ukimsumbua ni kama umekwisha kabisa.

Baba wa mtoto huyo, Joey anasema: “Ni kama alikuwa akisubiri kifo…mimi ni baba ambaye nilikuwa sitaki kumuona Papa.”

Joey anaelezea tukio la binti yake, Gianna kukutana na Papa ni kama muujiza ambao hakutarajia ungetokea.

Joey ameliambia Daily News kwamba alikuwa na wasiwasi mkubwa juu ya mfumo wa kinga wa binti yake, ambao tayari ulikuwa umedhoofika kwa matibabu ya mionzi na  kwa sababu hiyo alipinga binti yake kwenda kwenye mkusanyiko wa watu, hatua ambayo ingesababisha  hali yake kutetereka zaidi.

Lakini anasema madaktari ndio waliomtia moyo kwenda kumuona Papa.

Kwa mujibu wa mtandao wa PhillyVoice.com, uvimbe huo ulitokana na seli za damu kushambulia shina la ubongo wiki chache tu baada ya kuzaliwa.

Ugonjwa huo unadaiwa kuathiri kila mwaka watoto chini ya watano nchini Marekani.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles