27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Bunge ladoda, wabunge 85 wajadili bajeti

bungeniNa Arodia Peter, Dodoma

BUNGE la bajeti linaloendelea mjini Dodoma, jana limehudhuriwa na wabunge 85 badala ya 277 wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) baada ya wenzao wa Kambi ya Upinzani kususa vikao vinavyoendeshwa na Naibu Spika, Dk. Tulia Ackson kwa madai kuwa hawana imani naye.

Kwa wiki ya pili sasa wabunge hao wanaotokana na vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) huingia bungeni asubuhi na kutoka baada ya dua ya kuliombea Bunge hivyo kuwaacha wale wa CCM wakiendelea na mjadala wa bajeti peke yao.

Bunge la Jamhuri ya Muungano lina jumla wa wabunge 395, kati yao 118 ni kutoka vyama vya upinzani na 277 ni wa CCM wakiwamo wateule wa rais.

Katika mkutano huo wa tatu, kikao cha 43 cha Bunge la bajeti kilichoendelea jana, karibu robo tatu ya wabunge wa CCM hawakuwamo ukumbini huku wachangiaji walio wengi wakirudia michango ya wenzao waliotangulia.

Baadhi ya wabunge wa CCM waliozungumza na MTANZANIA kwa masharti ya kutotajwa majina gazetini, walisema kutokuwapo kwa wabunge wa upinzani katika mjadala wa bajeti kumesababisha Bunge hilo kupooza na kukosa msisimko wa hoja.

“Sitaki unitaje kwenye chombo chako, lakini wale wenzetu tumewa-miss, michango yao mara nyingi inalifanya Bunge kuwa hai zaidi, sifurahii hawa jamaa kukaa nje ya Bunge,” alisema.

Mbunge mwingine wa CCM kutoka mkoani Singida, alisema kabla hajaingia bungeni alikuwa anatamani kujenga hoja kama za Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (Chadema), hivyo kukosekana kwake kunamkosesha fursa ya kujifunza kutoka kwake.

Wakati hali ikiwa hivyo, juzi Mbunge wa Kasulu Mjini, Daniel Nsanzugwanko alimshauri Naibu Spika, Dk. Tulia pamoja na wabunge wa Ukawa kukaa chini na kumaliza tofauti zao ili kuweka taswira nzuri ya Bunge.

Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa alipoulizwa wanajisikiaje kuwa nje ya Bunge wakati wa kipindi hiki muhimu cha bajeti ya taifa, alisema ngoja CCM waendelee peke yao kwani hawaoni umuhimu wao.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles