31.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Bosi Zantel auawa na majambazi

Gabriel+PGOTOTunu Nassoro na Veronica Romwald, Dar es Salaam

MKUU wa Kitengo cha Mawasiliano wa Kampuni ya simu za mkononi ya Zantel, Gabriel Raphael, ameuawa kwa kupigwa risasi na watu wanaosadikiwa kuwa majambazi.

Tukio hilo la kusikitisha limegubikwa na utata, hasa baada ya watu hao kumuua mkuu huyo wa mawasiliano ndani ya gari yake na kuchukua bahasha ambayo inadaiwa ilikuwa na nyaraka muhimu na kuacha fedha.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camillus Wambura, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo katika eneo la Mikocheni jana saa 4:45 asubuhi.

“Ni kweli kuna mauaji yamefanyika katika eneo la Mikocheni jirani na Kiwanda cha Nabaki Afrika, kwa mujibu wa mashuhuda wamesema kwamba vijana wawili waliokuwa na pikipiki ndio waliotekeleza mauaji hayo,” alisema.

Kamanda Wambura alisema mashuhuda hao wamewaeleza askari wa jeshi hilo kwamba watu hao walipiga risasi kwenye vioo vya gari alilokuwa akiendesha Raphael kabla ya kutekeleza mauaji hayo.

“Walipiga risasi kwenye vioo hali iliyosababisha kuvunjika, kisha walimfyatulia risasi Raphael katika mkono na kwapa lake la kulia hali iliyosababisha apoteze maisha,” alisema.

Alisema mashuhuda hao walisema kwamba baada ya watu hao kutekeleza mauaji hayo, walichukua bahasha iliyokuwamo ndani ya gari hilo na kutokomea nayo kusikojulikana.

“Askari walifika katika eneo la tukio na walipoikagua gari ya marehemu, walikuta fedha kiasi cha shilingi milioni moja, simu pamoja na laptop yake, lakini mashuhuda wanasema waliondoka na bahasha,” alisema.

Alisema bado Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi wa tukio hilo ikiwamo kuanza msako dhidi ya watu hao wanaodaiwa kufanya mauaji.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles