25.2 C
Dar es Salaam
Monday, October 28, 2024

Contact us: [email protected]

Barabara Kinyerezi hadi Bonyokwa Kimara kujengwa kwa lami

Na Nora Damian, Mtanzania Digital

Wakazi wa Kata za Kinyerezi, Bonyokwa na Kimara jijini Dar es Salaam wataondokana na kero ya usafiri baada ya Serikali kujenga barabara kwa kiwango cha lami.

Barabara hiyo kilomita 7 inayoanzia katika Kata ya Kinyerezi kupitia Bonyokwa hadi Kimara itaanza kujengwa Desemba,2023.

Akizungumza jana Novemba 14,2023 wakati wa ziara ya kukagua barabara hiyo Waziri wa Ujenzi, Inocent Bashungwa, amesema tayari fedha zimetengwa kwa ajili ya ujenzi huo na kuiagiza Bodi ya Tanroad kukutana kwa dharura kuipitisha ianze kujengwa.

Mbunge wa Segerea, Bonnah Kamoli, akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kero wanazopata wananchi katika barabara ya Kinyerezi – Bonyokwa – Kimara baada ya Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa (Wapili kulia) kukagua. barabara hiyo.

“Naagiza Bodi ya Tanroad kama ni kikao cha dharura wakae wapitishe barabara ambayo maombi yameshaenda ikiwemo hii, baada ya mheshimiwa Rais Samia kutoa fedha sitaki nione vikao vya bodi vikiwa ni sababu ya kuchelewesha barabara hii kuanza,” amesema Bashungwa.

Msimamizi wa Kitengo cha Maendeleo Tanroads Mkoa wa Dar es Salaam, Mwanaisha Rajabu, amesema barabara hiyo imekuwa na changamoto kutokana na kuharibika mara kwa mara hasa kipindi cha mvua.

Amesema wako kwenye hatua za mwisho za manunuzi na kwamba ujenzi huo utahusisha kilomita 7 kwa upana wa mita 10.5 pamoja na daraja lenye urefu wa mita 25 na upana wa mita 10.

“Kutokana na changamoto hiyo Tanroads iliona barabara hii inapaswa kujengwa kwa kiwango cha lami kwa kuwa inahudumia wananchi wengi na ni barabara muhimu inayounganisha barabara ya Kinyerezi na Morogoro na kusaidia kupunguza foleni,” amesema Rajabu.

Katika hatua nyingine Waziri Bashungwa amewahakikishia wakazi wa Kata ya Tabata ambao wanatakiwa kuhama kupisha ujenzi wa miundombinu ya mabasi yaendayo haraka kuwa watalipwa fidia kwa mujibu wa sheria.

Baadhi ya wakazi hao wameiomba Serikali kuharakisha malipo ya fidia kwa kuwa wamesubiri kwa zaidi ya miaka miwili tangu walipofanyiwa tathmini.

Kwa upande wake Mbunge wa Segerea, Bonnah Kamoli, ameishukuru Serikali kwa jitihada za kuboresha miundombinu ya barabara hasa katika Kata ya Bonyokwa ambayo haina barabara za lami.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
591,000SubscribersSubscribe

Latest Articles