24.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

Bakwata wataka polisi kudhibiti wanaosherehekea Idd ufukweni

CHRISTINA GAULUHANGA Na AVELINE KITOMARY

-DAR ES SALAAM

SHEIKH wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhad Musa Salum, amewataka wazazi nchini kutowaruhusu watoto wao kwenda kusherehekea Sikukuu ya Idd ufukweni (Beach), huku akitaka Jeshi la Polisi kuchukua hatua kwa watakaokwenda kusherehekea kwenye maeneo hayo.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam, Sheikh Salum kwa niaba ya Mufti wa Tanzania, Sheikh Abubakari Zuberi, alisema imekuwa kawaida kwa wazazi kuruhusu watoto kwenda kusherehekea sikukuu katika maeneo ya ufukweni jambo ambalo linaweza kuchangia hata maambukizi ya Ukimwi.

Alisema ifike wakati mamlaka zinazohusika ikiwamo Jeshi la Polisi kuwachukulia hatua washerehekeaji ambao watakuwa wanatumia usafiri wa kukodi au binafsi kwenda katika maeneo hayo.

“Ninatoa wito kwa wazazi kuwazuia watoto wao kusherehekea sikukuu kwa namna hii, pia ninawaomba polisi kutumia nafasi zao kuwakamata wataokwenda kusherehekea ufukweni kwani huko ndiko wanakofanya maasi na kupoteza maana nzima ya sikukuu hii,” alisema Sheikh Salum.

Pia alisema kwa mwaka huu sherehe za Idd zitafanyika katika Viwanja vya Mnazi Mmoja kwa Mkoa wa Dar es Salaam.

Wakati huohuo, Baraza Kuu la  Waislamu Tanzania (Bakwata), limetangaza sherehe ya Idd el Fitr kitaifa kwa mwaka 2019 itafanyika mkoani Tanga.

Limesema swala ya Idd itafanyika katika Msikiti Mkuu wa Ijumaa uliopo Barabara ya 10, Ngamiani jijini Tanga kuanzia saa 1:30 asubuhi.

Baraza la Idd litafanyika katika ukumbi wa Tanga Beach Resort na mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.

Kuelekea sikukuu hiyo, MTANZANIA ilifanya uchunguzi katika baadhi ya masoko mbalimbali na kubaini bidhaa za vyakula bei zikiwa za kawaida huku nguo na viatu zimepanda.

Wakizungumza na MTANZANIA katika mahojiano maalumu kwa nyakati tofauti, baadhi ya wafanyabiashara walisema mbali ya wateja wengi kujitokeza katika masoko hayo, bado hali ya biashara si nzuri.

Mfanyabiashara aliyejitambulisha kwa jina la Abuu Mwarabu, alisema hali ngumu ya maisha imechangia biashara nyingi kudorora.

“Watu ni wengi sokoni, lakini hali ya biashara  haijachangamka, bado imedorora kutokana na ugumu wa maisha, hivyo biashara imekuwa ngumu kwetu, lakini tunajipa matumaini labda kesho (leo) mambo yatabadilika,” alisema Mwarabu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles