28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Bajeti yawagawa wabunge

bulaya-akitoa-maoniBAJETI Kuu ya Serikali iliyosomwa jana na Waziri wa Fedha, Saada Salum Mkuya, imewagawa wabunge ambapo baadhi wameiponda, huku wengine wakiisifia.
Baadhi ya wabunge hao wakiwamo wa vyama vya upinzani na chama tawala CCM, walisema bajeti hiyo haina jambo jipya na imezidi kuongeza mzigo wa umasikini kwa wananchi.

LUHAGA MPINA
Mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina (CCM), alisema kupandisha ushuru wa mafuta ya taa, petroli na dizeli ni kuongeza ugumu wa maisha kwa mwananchi kwa sababu ongezeko lolote kwenye mafuta hayo linaathiri moja kwa moja sekta ya usafirishaji.
“Bajeti haina lolote, ni kama ya miaka yote, kwa mfano hizo fedha wanazosema zitakwenda kwenye miradi ya umeme vijijini (REA) huwa haziendi. Tatizo la kushuka kwa thamani ya shilingi yetu kungesaidiwa na kushuka kwa bei ya mafuta nchini, lakini wao wameamua kupandisha mafuta,” alisema.
Mpina ambaye pia ni Mwenyeki wa Kamati ya Bunge Viwanda na Biashara, alisema katika bajeti nzima hakuna kifungu chochote kilichotengwa kwa ajili ya kulipa madeni ya wazabuni na makandarasi zaidi ya Sh bilioni 883.

OLE MEDEYE
Mbunge wa Arumeru Magharibi, Gudluck Ole Medeye (CCM), alisema bajeti imezingatia hali halisi na kupunguza utegemezi wa wahisani wa maendeleo nje ya nchi.
Hata hivyo, alisema: “Ili tuweze kupata umeme na maji vijijini lazima tujinyime kidogo ili tunufaike baadaye ingawa siungi mkono ongezeko la kodi kwa mafuta ya taa.”

HALIMA MDEE
Mbunge wa Kawe, Halima Mdee (Chadema), alisema bajeti haina jipya na zaidi imeondoa mamlaka ya Bunge kuhusika katika kuruhusu misamaha ya kodi.
“Mwaka jana walituletea bajeti ya jinsi hii, lakini utekelezaji wake ni chini ya asilimia 50, mara zote kutenga bajeti ni jambo moja na utekelezaji ni jambo jingine, hakuna unafuu,” alisema Mdee.

ESTHER BULAYA
Mbunge wa Viti Maalum, Esther Bulaya (CCM), ameonyesha wasiwasi kutokana na ongezeko la kodi katika mafuta.
Alisema licha ya fedha hizo kwenda katika Mfuko wa Mradi wa Umeme Vijijini (REA), lakini ongezeko hilo litamuumiza mwananchi wa kawaida.
“Kutokana na ongezeko hilo gharama za maisha zitapanda, bei za vitu zitaongezeka pamoja na gharama za usafiri,” alisema.

LIVINGSTONE LUSINDE
Mbunge wa Mtera, Livingstone Lusinde (CCM), alisema haungi mkono bajeti kupandisha bei ya mafuta ya taa kwa lengo la kuzuia uchakachuaji wa mafuta.
Alisema mafuta ya taa yamekuwa yakitumiwa na wananchi wengi, hasa vijijini hivyo hatua ya kupandisha bei ni sawa na kuwaongezea mzigo wa maisha.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles