31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Bageni akata rufaa kupinga hukumu ya kunyongwa

Kulwa Mzee, Dar es Salaam

Aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Kinondoni, Mrakibu wa Polisi (SP), Christopher Bageni, aliyehukumiwa kunyongwa hadi kufa kwa kuwaua wafanyabiashara wa madini kutoka Mahenge mkoani Morogoro, amepinga adhabu hiyo katika Mahakama Rufaa jijini Dar es Salaam.

SP Bageni amewasilisha maombi ya mapitio Mahakama ya Rufaa ya Tanzania ambayo yamepangwa kusikikizwa Juni 16, mwaka huu mbele ya jopo la majaji watatu, Stellah Mugasha, Ferdinand Wambali na Rehema Kerefu.

Katika maombi yake ya mapitio, Bageni amewasilisha sababu mbalimbali za kupinga adhabu hiyo ikiwamo kwamba jopo la majaji lilifanya makosa ya dhahiri katika muonekano na hivyo kusababisha haki kutozingatiwa katika kutoa hukumu hiyo.


SP Bageni alihukumiwa adhabu hiyo Septemba 16 mwaka 2016 na Mahakama ya Rufaa ya Tanzania mbele ya jopo la majaji watatu, Jaji Benard Luanda, Sauda Mjasiri na Semistocles Kaijage.

Mahakama ya Rufaa ilitoa hukumu hiyo baada ya kusikiliza rufaa iliyokatwa na Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP) akipinga aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Dar es Salaam (RCO) Kamishna Msaidizi wa Polisi, Abdallah Zombe na maofisa wenzake watatu akiwemo Bageni kuachiwa huru na Mahakama Kuu mwaka 2009.

Hukumu hiyo ilisomwa na aliyekuwa Msajili wa Mahakama ya Rufaa wakati huo, Jaji  John Kahyoza. Aliwataja wajibu rufani kuwa ni Zombe, SP Bageni, aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi wa Kituo cha Polisi Urafiki, Mrakibu Msaidizi wa Polisi (ASP) Ahmed Makelle na Rajabu Bakari.

Katika kesi hiyo, wafanyabiashara wa madini waliouwawa ni Sabinus Chigumbi, maarufu Jongo na ndugu yake, Ephrahim Chigumbi, Mathias Lunkombe na dereva taksi, mkazi wa Manzese Dar es Salaam, Juma Ndugu.

Walidaiwa kutenda makosa hayo Januari 14, mwaka 2006, katika Msitu wa Pande, uliopo wilayani Kinondoni baada ya kuwakamata wafanyabiashara hao Sinza, walipokuja Dar es Salaam kuuza madini.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles