26.1 C
Dar es Salaam
Thursday, September 19, 2024

Contact us: [email protected]

ATCL yapewa ujanja

Na Winfrida Mtoi, Mtanzania Digital

Shirika la Ndege Tanzania (ATCL),limeshauriwa kuongeza ununuzi wa ndege ndogo ili kuboresha sekta ya usafiri wa anga nchini.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Wajibu, inayojihusisha na kukuza mazingira ya uwajibikaji wa umma nchini,Ludovic Utoh, leo Septemba 13,2024 wakati akizindua Kitabu cha ATCL Business Model kinazozungumzia Hadithi ya Tamu na Chungu ya shirika hilo kilichoandikwa na waandishi wanne nguri ambao ni Jesse Kwayu, Neville Meena, Ansert Ngurumo na Absalom Kibanda.

Utoh ambaye aliwahi kuwa Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG), amesema ununuzi wa ndege ndogo utaleta manufaa makubwa kama vile kupanua wigo wa huduma za safari za ndani, ambapo abiria ataweza kufika kwa wakati na maeneo ambayo awali yalikuwa ni changamoto kufikika, pia itasaidia kupunguza muda wa safari.

“Ndege ndogo zina uwezo wa kufanya safari za mara kwa mara na kuwa na ratiba rahisi, tasaidia kupunguza ucheleweshaji wa safari, ATCL itakuwa na uwezo wa kutoa huduma kwenye maeneo ambayo kwa sasa hayana usafiri wa angani wa uhakika, hivyo kuongeza wigo wa huduma zake,” amesema Utoh.

Ameongeza kuwa ndege ndogo zina gharama nafuu za uendeshaji ikilinganishwa na ndege kubwa hivyo itaisadia ATCL kupunguza gharama na kuongeza faida.

Akizungumzia dhima ya kitabu hicho akichokizundua, amesema kina faida kubwa kwa ATCL na sekta ya usafiri wa anga nchini, kutokana na kutoa uchambuzi wa kina kuhusu historia ya shirika na changamoto za kiutendaji.

Amesema kimetoa mapendekezo ya muhimu kuhusu jinsi ATCL inavyoweza kuboresha uendeshaji wake, ikiwa ni pamoja na marekebisho ya mikataba, ununuzi wa ndege ndogo, na kuiga mifano bora kutoka kwa mashirika mengine kama Ethiopian Airways.

Ameongeza kuwa kitabu kimeeleza mapungufu katika ununuzi wa ndege, na kutoa mwanga kuhusu mikakati ya usimamizi wa ndege, kwa kuhakikisha ununuzi unafanywa kwa njia bora, yenye ufanisi, na kwa kutumia rasilimali zilizopo kwa tija.

“Kupitia kitabu hiki kimetusaidia kuona umuhimu wa kufuata viwango vya kimataifa katika ununuzi wa ndege na usimamizi wa shughuli za ndege, itasaidia ATCL na mashirika mengine ya ndege nchini kujiweka katika nafasi nzuri kwenye soko la kimataifa na kuhakikisha kuwa wanatoa huduma zinazokubalika kimataifa aidha kinachangia kukuza uwajibikaji wa umma kwa kutoa mapendekezo ya uboreshaji katika usimamizi na utendaji wa shirika,” amesema Utoh.

Akizungumzia changamoto za usafiri wa anga nchini, amesema ATCL katika mkataba wake na sekta ya usafiri wa anga nchini ( (TFFA) wanapaswa kufanya marekebisho katika mkataba wake wa kuendesha shughuli za usafirishaji kwa kuangalia masharti ya ununuzi wa ndege zinapaswa kuzingatia viwango vya kimataifa na kuhakikisha ufanisi wa ndege na kuangalia gharama za uendeshaji.

Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Media Brain, Jesse Kwayu ambaye ni miongoni mwa walioandika kitabu hicho, amesema, uandishi wa vitabu ni eneo muhimu la kutunza kumbukumbu juu ya masuala mbalimbali yaliyotokea na yanayotokea nchini.

Amesema waandishi wengi wana mambo mengi kichwani ambayo wangeyaandika yangelisaidia taifa, amedai kwa kutambua faida za vitabu, Kampuni ya Media Brain, wameamua kubeba jukumu la kuwasilisha maarifa na ujuzi wao kwa kuandika vitabu ili kuwasaidia wengine.

Naye Mkurugenzi Mwenza wa Kampuni hiyo, Neville Meena, amesema ni kitabu cha pili wanakiandika na kukichapisha, wamefanya utafiti na uchambuzi kuhusu ajenda walizozikusudia ili kuleta dhana ya uwajibikaji.

“Kitabu cha kwanza kilikuwa kilichoangazia utawala wa Dk. Magufuli cha pili kinasimulia ‘Hadithi ya Matamu na Machungu’ ya shirika la Ndege Tanzania tangu kuanzishwa kwake mwaka 1977 hadi sasa mafanikio na changamoto zake,” amesema Meena.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
589,000SubscribersSubscribe

Latest Articles