30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

AFANDE SELE AJITOA ACT- WAZALENDO

Afande Sele
Afande Sele

Na ELIZABETH HOMBO-DAR ES SALAAM

ALIYEWAHI kuwa mgombea ubunge wa Morogoro Mjini kupitia Chama cha ACT-Wazalendo, Selemani Msindi maarufu Afande Sele, amejivua uanachama wa chama hicho.

Uamuzi huo wa Afande Sele unakuja ikiwa ni siku chache tangu aliyekuwa Katibu wa Kamati ya Mipango, Habib Mchange kujivua uanachama na kutangaza kuachana na siasa.

Taarifa ya Afande Sele kujivua uanachama wa chama hicho, aliiweka katika ukurasa wake Facebook.

Itakumbukwa kuwa katika siku za karibuni Afande Sele amekuwa akieleza kutoridhishwa na viongozi wa ACT-Wazalendo, akisema msimamo wao umekuwa haueleweki.

Kutokana na hilo, alisema anashindwa kujua iwapo msimamo wa chama hicho ni kuunga mkono upinzani au CCM.

Katika taarifa yake ya jana, Afande Sele alisema ameamua kuchukua uamuzi huo kwa sababu Katiba ya nchi inamruhusu.

“Habari za wakati huu ndugu zangu, naamini tupo pamoja katika kujitafutia maisha na kulijenga taifa letu pendwa Tanzania ambalo ndani ya Katiba yake kuna kipengele muhimu kinachotupa uhuru kwa kila mtu kufanya mambo yake apendavyo ilimradi tu havunji sheria za nchi.

“Sasa kwa kuzingatia uhuru huo tuliopewa na Katiba yetu leo (jana) natangaza rasmi kujivua uanachama wa Chama cha ACT-Wazalendo na kutokuwa mfuasi wa chama chochote cha siasa bali nitabaki kuwa raia wa kawaida ndani ya nchi yetu huku nikiendelea na majukumu yangu mengine ya kimaisha mpaka hapo nitakapoamua vingine kama nitakuwa na sababu ya kufanya hivyo.

“Nawatakia kila la kheri wote waliobaki ndani ya chama pia nawatia moyo mkuu wa kuendeleza harakati za ujenzi wa chama ili kuleta upinzani sahihi na imara utakaosaidia kujenga taifa kwa faida yetu na vizazi vijavyo.

“Naomba ieleweke kuwa uamuzi huu sijauchukua kwa bahati mbaya hivyo naomba kila mmoja awe wa ndani au wa nje ya chama chetu aheshimu uamuzi wangu kama mimi ninavyoheshimu maamuzi ya watu wengine kwa mujibu wa Katiba ya nchi inavyosema…Ahsanteni sana wadau tukutane maishani,”alisema Afande Sele.

Mbali ya Afande Sele na Mchange, Novemba 20 mwaka huu mbunge wa zamani wa Kasulu Mjini, Mosese Machali naye alijitenga na chama hicho.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles