Na Willbroad Mathias, DAR ES SALAAM
TRENI ya abiria inayofanya safari zake kati ya Kituo Kikuu cha Reli na maeneo ya Pugu  Dar es Salaam maarufu kama ‘Treni ya Mwakyembe’ nusura ichomwe moto juzi, baada ya wananchi   kudai kuchoshwa na usumbufu wa shirika hilo.
Wananchi hao walitaka warudishiwe nauli zao kwa kile walichodai Shirika   la Reli Tanzania (TRL) limeshindwa kuwa na ratiba inayoeleweka.
Tukio hilo lilitokea juzi saa 3:00 usiku eneo la Majumbasita, baada ya treni hiyo kukaa kituoni hapo kwa muda mrefu bila kuambiwa kuambiwa chochote.
Hali hiyo iliwafanya abiria  kuvamia kituo kidogo cha mawasiliano kilichopo eneo hilo wakitaka warejeshewe  nauli zao vinginevyo wangekichoma moto pamoja na mabehewa ya treni hiyo.
MTANZANIA liliwashuhudia abiria   wakitaka kuingia ndani ya kituo hicho huku wakiwalazimisha wafanyakazi waliokuwapo wawarudishie fedha zao za nauli.
Purukushani hiyo iliyodumu kwa takribani saa mbili  ilimalizika kwa abiria hao kuvunja vioo vya mabahewa ya treni vipatavyo 30.
Wafanyakazi kuona hivyo walijifungia ndani ya kituo hicho  huku  polisi waliokuwa wakisindikiza treni hiyo wakitimua mbio   kunusuru maisha yao.
Baadhi ya abiria walisema   tangu Ijumaa   iliyopita wamekuwa wakipata usumbufu kwa kukatishiwa tiketi huku treni  ikichelewa na wakati mwingine kutoonekana kabisa.
Walisema  jambo hilo  limekuwa likiwasababishia hasara na kuwalazimu  kutafuta usafiri mwingine na   kuchelewa kufika  kwenye majukumu yao.
Rashid Mpalamo mkazi wa Pugu alisema alipanda treni hiyo saa 2:30 usiku kwenye Kituo cha Reli Stesheni, lakini baada ya kufika Majumbasita waliambiwa wasubiri kwa kile kilichodaiwa kuwa   treni ya mizigo ilikuwa imeanguka maeneo ya Pugu.
Meneja wa kituo hicho, Benedict Kassege alisema  anashangazwa na kitendo cha abiria hao kuwavamia akidai kuwa wao hawahusiki na ukatishaji tiketi bali wanachokifanya ni mawasiliano ya njia hiyo.