30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

YANGA VS NAMUNGO LEO: Iwe kwa jua, mvua lazima mtu afe

NA MWANDISHI WETU-DAR ES SALAAM

MABINGWA wa kihistoria wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga, wametoa tahadhari kwa Namungo FC, wakiwaambia wasipoangalia wanaweza kupata aibu ya mwaka kutokana na kipigo walichowaandalia katika uwanja wao wa nyumbani.

Kikosi cha Yanga leo kinawakabili Namungo katika michuano ya Kombe la Shirikisho (ASFC) hatua ya 16 bora kwenye Uwanja wa Kassim Majaliwa.

Kocha Mkuu wa Yanga, Mwinyi Zahera, alisema licha ya kwamba mchezo huo utakuwa mgumu kutokana na kucheza uwanja wa ugenini, lakini amewaandaa vizuri vijana wake kuhakikisha wanapata matokeo mazuri.

“Hautakuwa mchezo rahisi kwani tupo uwanja wa ugenini ila kwa namna tulivyofanya maandalizi, nina imani tutapata matokeo mazuri na kutinga hatua inayofuata.

“Ubaya wa michuano hii ni kwamba timu inayofungwa inaondoka, hakuna kujiuliza kwamba tutarudiana, wachezaji wangu wanalitambua hilo na wameahidi kuwapa raha mashabiki,” alisema.

Kwa upande wake kocha Mkuu wa Namungo FC, Bakari Malima, alisema licha ya kwamba Yanga ni timu kubwa, lakini wao hawaogopi na wanachokitaka ni kuibuka na ushindi ikizingatiwa wapo uwanja wa nyumbani.

“Vijana wangu wanafahamu kwamba wanakutana na timu kubwa, lakini nimewaambia wasiwe na wasiwasi wowote na wao wameniahidi kwamba watapambana vilivyo.

“Kama Yanga watauchukulia mchezo huu kirahisi, nadhani wanaweza wakajikuta wanapata aibu kwani hata sisi tumejiandaa kukabiliana nao kwa kila namna,” alisema. 

Yanga ilitinga hatua hiyo ya 16 bora walipowafunga Biashara United ya Mara kwa mikwaju ya penalti 5-4, baada ya kumaliza dakika 90 zikifungana mabao 2-2 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Kwa upande wao, Namungo waliwafunga Mighty Elephant bao 1-0 na sasa wanawakabili Yanga kuona namna ya kutinga robo fainali.

Bingwa wa michuano hiyo ndiye atakayeiwakilisha nchi katika Kombe la Shirikisho barani Afrika msimu unaokuja, huku timu zote zilizopo hatua hiyo ya 16 bora zikitaka kupata heshima hiyo.

Yanga wataingia kwenye mchezo huo wakitoka kushinda mabao 2-1 dhidi ya Mbao FC ugenini, mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliochezwa Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.

Hata hivyo, bado Wanajangwani hao wanazo hasira za kufungwa bao 1-0 na watani zao wa jadi Simba, mchezo wa Ligi Kuu na kama Namungo watakaa vibaya, wanaweza kushushiwa mvua ya mabao.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles