24.8 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

WAFICHA TAKWIMU ZA KIPINDUPINDU KWA HOFU YA KUTUMBULIWA

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu

NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM

BAADHI ya watendaji wa halmashauri mbalimbali nchini wamegundulika kuficha takwimu za wagonjwa wa kipindupindu kwa hofu ya kutumbuliwa na Rais Dk. John Magufuli.

Halmashauri hizo hutumia mbinu ya kuwachanganya wagonjwa wa kipindupindu na wale wasiokuwa nao katika wodi moja ili kuficha ukweli.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu alisema hayo jana alipozungumza na waandishi wa habari kuhusu mwenendo wa ugonjwa huo kwa kipindi cha wiki iliyoanzia Novemba 21 hadi 30, mwaka huu.

“Inasikitisha, wagonjwa wa kipindupindu wanachanganywa na wale wasiokuwa nacho, hili ni kosa la jinai, kuwachanganya pamoja kunaongeza uwezekano wa wale wasiokuwa na ugonjwa huo kuambukizwa haraka na wenzao.

“Leo (jana) sizitaji halmashauri zinazofanya hivyo lakini iwapo wataendelea kuwachanganya wagonjwa kwa kuhofia  kutumbuliwa, nitaenda kuwaripoti ngazi ya uteuzi,” alionya.

Waziri Ummy alisema katika wiki hiyo kumeripotiwa jumla ya wagonjwa 458 katika mikoa sita na vifo vya watu tisa.

“Mkoa wa Morogoro kumeripotiwa wagonjwa 282, Dodoma 196 na vifo viwili, Mara wagonjwa 81, Kigoma wagonjwa 30 na vifo vine, Arusha wagonjwa 11 na Dar es Salaam wagonjwa wanane,” alisema.

Alizitaka kamati za ulinzi na usalama za kila kata kuingiza agenda ya kipindupindu katika vikao vyao kuongeza nguvu ya mapambano.

“Wajadili wajue wamefikia wapi katika kukitokomeza, kamati za afya za kata nazo zihakikishe kila kaya inakuwa na choo bora ndani ya miezi sita kuanzia sasa maana hali ni mbaya.

Awali, waziri huyo alipokea msaada wa mashine 15 ambazo zitatumika kutibu mabadiliko ya awali ya saratani ya shingo ya kizazi zilizotolewa na Shirika lisilo la Serikali la Pink Ribbon & Red Ribbon.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles