27.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 18, 2024

Contact us: [email protected]

Ulinzi wazidi kuimarishwa kesi za ugaidi

NA ELIYA MBONEA, ARUSHA
JESHI la Magereza mkoani hapa limezidi kuimarisha ulinzi ndani na nje ya majengo ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, wakati wa kesi za watuhumiwa 60 wa matukio tofauti ya kigaidi.

Wakati ulinzi ukiimarishwa, mtuhumiwa mpya wa matukio ya kigaidi, Buchumi Hassan, amepandishwa kizimbani kusomewa mashtaka yake na kuunganishwa na watuhumiwa wenzake 60 na kufanya idadi yao kufikia 61.

Kwa wiki kadhaa sasa kulikuwa na ulinzi mkali wa askari magereza eneo hilo wakati wa kuleta watuhumiwa na kuwaondoa eneo la mahakama na ndugu zao wamezuiwa kuingia ndani kwasababu za usalama.

Baadhi ya askari magereza wanaokuwa doria eneo ambalo watu wenye kesi hukaa kusubiria kuitwa wamejikuta wakizuiwa kutumia simu pindi watuhumiwa wanapokuwa eneo hilo la mahakama.

Mwandishi wa habari hizi alikuwa ni moja ya baadhi ya watu waliozuiwa kutumia simu katika eneo hilo.

“Tunaomba ukiwa eneo hili usitumie simu yako tafadhali sana,” alisikika askari magereza mmoja aliyekuwa doria.

Kesi zote zinazowakabili watuhumiwa hao ziliahirishwa na Hakimu Mkazi Devotha Msofe baada ya Mwendesha Mashtaka wa Serikali, Agustone Kombe, kudai upelelezi bado haujakamilika.

Watuhumiwa hao wameshtakiwa kwa makosa yaliyo chini ya Sheria ya Kuzuia Ugaidi na Sheria namba 22 ya mwaka 2002 inasema upelelezi wa shauri hilo ukishakamilika, Mahakama Kuu ndiyo yenye mamlaka ya kusikiliza na kutoa uamuzi.
Watuhumiwa hao 60 waliopo katika kesi mbalimbali wanakabiliwa na mashtaka ya kuua, kujaribu kuua, kusajili na kusafirisha vijana kujiunga na Al-Shabaab.

Mbali na mashtaka hayo, wanahusishwa na tukio la milipuko ya mabomu Baa ya Arusha Night Park, mlipuko wa bomu Viwanja vya Soweto na mlipuko uliotokea Kanisa la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi Olasite jijini Arusha uliosababisha vifo na majeruhi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles